Siasa

Utata mwingine ODM makundi mawili yakipanga NDC sambamba

Na MOSES NYAMORI March 17th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

VITA vya kung’ang’ania mamlaka ndani ya ODM vimechukua mwelekeo mpya baada ya mrengo wa Linda Mwananchi kutangaza kuwa utakuwa na Kongamano sambamba wa Wajumbe (NDC) mnamo Machi 27.

Kinara wa ODM Dkt Oburu Oginga anatarajiwa kuongoza NDC siku hiyo huku kambi ya Linda Mwananchi ikisisitiza ndiyo ina wajumbe halali wa ODM katika kongamano jingine watakaoliandaa siku hiyo.

Mirengo yote miwili bado haijatangaza mahali ambapo wataandaa makongamano yao.

Dkt Oginga na mrengo wake wanataka maafisa wapya wa chama waidhinishwe katika NDC yao.

Maafisa hao ni manaibu kiongozi wa chama Godfrey Osotsi, Abdulswamad Nassir na Simba Arati pamoja na Mwenyekiti wa chama Gladys Wanga.

Hata hivyo, Linda Mwananchi inayoongozwa na Seneta wa Nairobi Edwin Sifuna nayo inataka NDC itakayoandaliwa, itumike kuwachagua viongozi wapya.

Wakitangaza NDC ya Dkt Oburu kuwa haramu, mrengo wa Bw Sifuna pia umezua maswali kuhusu orodha ya wajumbe watakaoshiriki kwenye kongamano lenyewe.

“Hiyo NDC ya Linda Ground ni haramu, haizingatii sheria na inalenga kutimiza ajenda za kisiasa. Mkutano huu unapangwa na Kiongozi wa UDA Rais William Ruto na hilo linathibitisha kuwa ODM sasa inasimamiwa kutoka Ikulu,” Bw Osotsi akaeleza Taifa Leo jana.

Alifichua katika NDC ya Linda Mwananchi watawachagua viongozi wapya wa ODM.

“Tutakuwa na NDC yetu ambayo itahudhuriwa na wanachama halisi wa ODM. Ni wajumbe na wanachama hawa ndio watatoa mwelekeo wa kulinda chama na falsafa ya uongozi wa Raila Odinga,” akaongeza akisema kuwa viongozi mbalimbali tayari wameonyesha nia ya kuhudhuria kongamano lao.

Seneta huyo wa Vihiga anahoji kuwa Dkt Oginga angemakinikia kumaliza mzozo ndani ya chama hicho kupitia upatanishi badala ya kuandaa kongamano linaloegemea mrengo mmoja.

Hata hivyo, Mbunge wa Nyando Jared Okello alisema sheria inasisitiza mwanya wa siku 21 kabla ya kuandaliwa kwa NDC kwa hivyo, haiwezekani mrengo wa Linda Mwananchi kuwa na kongamano lao siku hiyo hiyo.

Aliongeza kuwa NDC inaweza kuandaliwa baada ya uamuzi wa Baraza Kuu la Chama (NEC) pekee.

“Walitoa notisi ya siku 21 wapi? Sasa wamegeukia kioja ambacho hakitambuliwi kisheria,” akasema Bw Okello.

Kando na NDC sambamba, Dkt Oburu na kundi lake pia wanapambana mahakamani kushinda kesi ambayo imewasilishwa kuzima kongamano hilo.

Mwanachama wa ODM Vincent Chepkwony kupitia Kampuni ya Mawakili ya Kimani & Murithi aliandikia chama na kuzua maswali kuhusu uhalali kwa kongamano hilo na orodha ya wajumbe.

Bw Chepkwony anadai kuwa notisi ya kuandaliwa kwa kongamano hilo ilitolewa na Naibu Katibu Mkuu badala ya Katibu Mkuu, hali ambayo anasema inakiuka Katiba ya ODM.

Hata hivyo, Kiongozi wa Wachache Bunge la Kitaifa Junet Mohamed amehusisha kesi hiyo na mrengo wa Bw Sifuna na Gavana wa Siaya James Orengo.