Vifungu vya katiba ya ODM vinavyotishia kusambaratisha NDC ya Machi 12
KONGAMANO la wajumbe wa ODM (NDC) la Machi 27 limegeuka jukwaa la vita vya kisheria na huenda likayumbisha chama hicho baada ya kifo cha Raila Odinga.
Hii ni baada ya Kampuni ya Uwakili inayowakilisha mwanachama wa ODM Vincent Chepkwony kuzua maswali kuhusu uhalali wa kisheria wa kongamano hilo.
Chepkwony anadai kuwa notisi ya kuandaliwa kwa NDC ilitolewa na Naibu Katibu Mkuu badala ya katibu mkuu jinsi ambavyo imenakiliwa kwenye Katiba ya ODM.
Kifungu cha 49 cha Katiba ya ODM kinasema kuwa Kongamano Spesheli la Wajumbe wa chama litaitishwa na Mwenyekiti kupitia uamuzi wa Kamati ya Kitaifa ya Chama au kupitia ombi la theluthi moja ya wajumbe wanaostahili kuhudhuria mkutano huo.
Katiba hiyo hiyo inasema notisi na ajenda ya mkutano huo itatumwa na Katibu Mkuu zaidi ya siku 21 kabla ya tarehe hiyo na pia kuchapishwa katika mtandao wa chama.
Aidha, notisi na ajenda hiyo lazima ichapishwe katika gazeti moja la Kingereza au idhaa moja ya Kiswahili.
Bw Chepkwony pia amezua maswali kuhusu uhalali wa kisheria wa orodha ya wajumbe ambao wanatarajiwa kuhudhuria kongamano hilo.
Anadai kwamba kaunti nne ambazo ni Migori, Kisumu, Nairobi na Taita Taveta bado hazijaandaa chaguzi zao za mashinani.
“Kila kamati shirikishi ya kaunti inatarajiwa kuwateua wawakilishi wao mahali ambapo wawakilishi ni gavana, mbunge au mbunge mwakilishi wa kike wanashikilia nyadhifa chamani. Nani sasa atawateua?” akauliza Bw Chepkwony kupitia kampuni ya uwakili ya Kimani na Muriithi.
Pia mlalamishi huyo anasema hakuna uchaguzi ambao umefanywa kwa vuguvugu la viongozi wanawake wa ODM pamoja na vuguvugu la walemavu.
Maafisa wa vuguvugu la wanawake na walemavu wote ni wajumbe wa NDC.
“Wanachama wengine wanataka kufahamu nani atakuwa akiwawakilisha katika kongamano hilo,” akaongeza.
Kiranja wa Wengi Junet Mohamed alihusisha kesi hiyo na kundi pinzani la wananchi linaloongozwa na Seneta wa Nairobi Edwin Sifuna na Gavana wa Siaya James Orengo.
Alidai wanasiasa hao sasa wanawatumia washirika kujaribu kuzima NDC hiyo.
“Mbona sasa wanaelekea Mahakamani? Waliambia Oburu aandae NDC na sasa notisi imetolewa na wanajaribu kuzima kongamano hilo. ODM ni chama kinachofuata sheria na hatuwezi kusimamishwa na watu watano,” akasema Bw Mohamed.
Seneta wa Vihiga Godfrey Osotsi ambaye ni wa mrengo wa Linda Mwananchi alikanusha kuwa wanalenga kusimamisha NDC ila wanataka nafasi za uongozi ziwe wazi ili kuwe na uchaguzi wa washikilizi wapya.