Viongozi wa ODM Pwani wasisitiza ‘pawa si pawa bila Joho’
VIONGOZI wa kisiasa kutoka eneo la Pwani wameongeza wito wa kutaka uwakilishi mkubwa zaidi katika ngazi za juu za serikali, wakisisitiza kwamba Waziri wa Madini Hassan Joho awe mgombea mwenza wa Rais William Ruto katika uchaguzi wa 2027.
Wakizungumza wakati wa Idd Baraza jijini Mombasa, viongozi hao walieleza kwamba msukumo wao si wa tamaa ya mamlaka, bali mkakati mpana wa kusawazisha uongozi wa nchi.
Walisisitiza umuhimu wa uwakilishi wa kidini na kikanda katika serikali ya kitaifa.
Waliohutubu walilalamika kwamba Pwani imekuwa ikitengwa kwa muda mrefu katika uongozi wa juu, wakidai kuwa nafasi ya juu zaidi ambayo eneo hilo hupewa ni ya uwaziri.
“Tulishawahi kutoa mawaziri, lakini sasa tuna mtoto wa nyumbani mwenye mvuto wa kitaifa. Ni jukumu letu kumsukuma mbele,” alisema Mbunge wa Kisauni, Bw Rashid Bedzimba, akitoa wito wa umoja.
Hoja hiyo iliungwa mkono na wengi, huku wanasiasa hao wa ODM wakisisitiza kuwa mazungumzo ya kisiasa na kambi ya Rais Ruto kabla ya uchaguzi ujao lazima yawe na matokeo ya kugawana mamlaka makuu.
“Ndani ya ODM tunaambiwa kutakuwa na mazungumzo. Ikiwa UDA itachukua urais, basi ODM lazima ichukue nafasi ya pili, na nafasi hiyo ije Pwani,” alisema Mbunge wa Likoni, Bi Mishi Mboko.
Alikosoa kile alichokiita mtazamo wa kujidharau miongoni mwa baadhi ya wanasiasa, wanaoamini kuwa eneo hilo halijakomaa kisiasa kutoa Naibu Rais.
Mbunge huyo aliongeza kuwa ni Waziri huyo wa Madini pekee aliyeonyesha uwezo wa kupigania maslahi ya Pwani katika serikali ya kitaifa iwapo atapata nafasi ya kufanya maamuzi ya kitaifa.
Mbunge wa Changamwe, Bw Omar Mwinyi, alipendekeza wazo la kusawazisha uongozi kwa misingi ya dini. Alisema Kenya inapaswa kuzingatia mfumo ambapo Rais na Naibu wake wanawakilisha jinsi nchi ina dini tofauti.
“Ikiwa Rais ni Mkristo, basi Naibu wake awe Muislamu,” alisema, akitoa mifano ya nchi nyingine ambapo usawa huo huonekana katika uongozi wa juu.
Gavana wa Mombasa, Bw Abdulswamad Nassir, alisisitiza kuwa wakati ODM iliingia katika mpangilio wa serikali jumuishi na UDA, walikubaliana kuanzisha mazungumzo ya muungano kabla ya 2027.
Naibu kiongozi huyo wa chama cha ODM alisema hawatalegeza kamba kwa msimamo wao wa kutaka nafasi ya Naibu Rais.
“Dai letu lisilobadilika ni kwamba nafasi ya Naibu Rais lazima ije ODM. Na kama viongozi wa Pwani tunasisitiza kuwa mgombea mwenza atoke eneo hili,” alisema.
Bw Joho aliepuka kutangaza wazi msimamo wake kuhusu nafasi hiyo inayoshikiliwa kwa sasa na Profesa Kithure Kindiki, ambaye anaungwa mkono na viongozi wa UDA kutafuta muhula wa pili.
Badala yake, alizungumzia azma yake ya baadaye ya urais.
Bw Joho pia alithibitisha uaminifu wake wa muda mrefu kwa marehemu Raila Odinga na mizizi yake ndani ya ODM, akijieleza kama mwanachama mwanzilishi anayeelewa mwelekeo wa chama hicho.
Pia aliwapuuza wakosoaji wa serikali akisema wanafuata maslahi yao binafsi, na akawataka wafuasi kuzingatia malengo ya kudumu.