Washirika wa Ruto wampangia Natembeya katika pambano kali la kumpokonya ugavana 2027
KAMPENI za kuwania kiti cha ugavana Kaunti ya Trans Nzoia mwaka 2027 zimeanza kushika kasi huku wandani wa Rais William Ruto wakijipanga kumng’oa Gavana George Natembeya katika pambano linalotarajiwa kuwa kali kati ya muungano wa Kenya Kwanza na ule wa upinzani.
Ushindani huo sasa unaonekana kuchukua mwelekeo, wagombea watatu wakitangaza azma ya kumng’oa Bw Natembeya ambaye angali na ushawishi mkubwa mashinani.
Hata hivyo, Bw Natembeya anakabiliwa na shinikizo inayoongezeka kutoka kwa viongozi wa Kenya Kwanza wanaomlaumu kwa utendakazi duni, siasa za mgawanyiko na kushindwa kushirikiana na serikali kuu hata ingawaje, amekanusha vikali madai hayo.
Miongoni mwa wanaowania kiti hicho ni Balozi wa Kenya katika UN-Habitat na aliyekuwa Waziri wa Afya, Susan Nakhumicha, aliyekuwa Mbunge wa Kiminini Chris Wamalwa, na Mbunge wa sasa wa Kiminini Kakai Bisau.
Wote wameongeza kasi ya kampeni zao wakijitambulisha kama watakaoleta mabadiliko huku wakiegemea ajenda ya maendeleo ya serikali ya kitaifa.
Akizungumza katika ibada ya kanisa eneo la Chebarus, Cherangany, Bi Nakhumicha alitangaza rasmi azma yake ya kuwania ugavana, akisema yuko tayari kuwahudumia wakazi wa kaunti hiyo.
“Naomba wananchi wa Trans Nzoia wanipatie nafasi ya kushughulikia changamoto zinazowakumba. Niko tayari kufanya kazi na kuhakikisha huduma bora,” alisema.
Alidai kuwa kaunti hiyo imeachwa nyuma kutokana na uhusiano mbaya kati ya serikali ya kaunti na ile ya kitaifa.
Aidha, alisisitiza kuwa hataogopa vitisho vya kisiasa, akiongeza kuwa ana uwezo na maono ya kuongoza kaunti hiyo bila kujali jinsia yake.
Kwa upande wake, Bw Bisau alipuuza rekodi ya maendeleo ya Bw Natembeya, akisema ni wakati wa kubadilisha mwelekeo wa kaunti hiyo na kufungua milango ya maendeleo.
Naye Dkt Wamalwa, ambaye alikuwa mpinzani mkuu wa Bw Natembeya katika uchaguzi wa 2022, anajaribu tena bahati yake baada ya kushindwa, huku akilenga kuimarisha nafasi yake kisiasa.
Viongozi wa Kenya Kwanza wameongeza mashambulizi dhidi ya Bw Natembeya, wakimlaumu kwa kuunga mkono siasa za upinzani na kudhoofisha maendeleo ya kaunti.
Hata hivyo, Gavana Natembeya amejibu mashambulizi hayo kwa kuwapuuza wapinzani wake akiwataja kama vibaraka wa kisiasa wasioweza kubadili mwelekeo wa kura.
Pia amelaumu Wizara ya Fedha kwa kuchelewesha fedha za kaunti, akisema hali hiyo imeathiri utekelezaji wa miradi ya maendeleo.
“Sihitaji kufanya kazi na Rais ili kaunti ipate fedha. Hii ni haki ya kikatiba na serikali ya kitaifa lazima iheshimu ugatuzi,” alisema.
Aidha, alidai kuwa amekuwa akilengwa kisiasa kutokana na msimamo wake wa kutetea maslahi ya eneo la Magharibi.
Uchaguzi wa 2027 unapokaribia, pambano hilo linatarajiwa kuwa kali huku kila upande ukijipanga kuvutia wapiga kura katika kaunti hiyo muhimu ya kisiasa.