Wasuka mikakati kuhama Kenya Kwanza
WIMBI la Wabunge na wanasiasa wanaounga Serikali ya Kenya Kwanza kuhamia upinzani kabla ya Uchaguzi Mkuu wa 2027 linavuma kote nchini wakilenga kuokoa maisha yao ya kisiasa, wachambuzi wa siasa wanasema.
Wengi wao tayari wameanza kuweka mikakati chini ya maji kuhama muungano tawala, kulingana na washirika wao.
Inasemekana kuwa zaidi ya wabunge 100, hasa kutoka Mlima Kenya na Magharibi mwa Kenya, wamekuwa wakifanya mikutano ya faragha na wafuasi wao wa mashinani pamoja na washauri wao wa kisiasa.
Lengo lao ni kujiandaa kwa mabadiliko ya kisiasa yanayoweza kutokea kutokana na hali ya kutoridhika inayozidi kuongezeka dhidi ya utawala wa Ruto katika maeneo wanayowakilisha.
Inadaiwa kuwa wabunge hao wamekuwa wakifuatilia hali mashinani na kupima upepo wa kisiasa, hasa baada ya maamuzi tata ya sera, hatua zisizopendwa za ushuru, na hali ya chuki inayoongezeka mashinani.
Wachambuzi wa siasa wanasema kuwa si jambo jipya wimbi la wanasiasa kuhama vyama kushuhudiwa katika mazingira kama ya sasa lakini kuelekea 2027 litakuwa na nguvu.
“Idadi kubwa ya wabunge wa sasa wana kibarua cha kujikomboa na kurejesha ushawishi wao. Wamekuwa wakijitenga na wananchi na kufumbia macho hali halisi inayokumba raia. Hali hii huenda ikawagharimu sana,” anasema mchanganuzi wa siasa Dkt Isaac Gichuki.
Anasema kwamba hali ya raia kutoridhika na serikali ya Rais Ruto, huenda ikaathiri pakubwa wabunge wanaomuunga mkono.
Mchanganuzi huyo anasema hisia za raia ni kuwa wabunge wamewasaliti kwa kutosikiliza kilio chao huku wakiunga serikali inayowakandamiza kwa sera zake.
Duru zinasema kuwa wabunge wanaounga serikali wana presha kutoka kwa wapiga kura hali ambayo imewalazimisha kuwazia kubadilisha mikakati wakilenga kuhama muungano tawala.
Idadi kubwa ya wapiga kura katika Mlima Kenya, ambalo awali lilionekana kuwa ngome ya Ruto, wameripotiwa kutoridhishwa na kile wanachokiita usaliti na kutengwa licha ya kumchagua Rais kwa wingi mwaka wa 2022.
Inasemekana baadhi yao wanazungumza lugha tofauti wakiwa mashinani huku wakionekana kuunga serikali.
“Mashinani, tunafanya siasa zetu. Nimewaeleza wazi kuwa wakati ukifika, nitawapa mwelekeo mpya na ni wazi kuwa hatutaiunga mkono serikali hii tena,” mbunge mmoja aliambia Taifa Jumapili na kuomba asitajwe jina kwa sababu ya ukuruba wake na serikali.
Anasema wananchi wengi wanalalamika kuwa utekelezaji wa sheria kali za ushuru, ukatili dhidi ya wanaokosoa serikali na ukosefu wa usawa katika uteuzi serikalini zimewakera raia wengi.
“Wengine wanaojifanya kuunga mkono ajenda ya Rais hadharani wamekuwa wakitufuata kwa siri na kutuambia kuwa wamo serikalini kwa sasa kwa ajili ya kula tu, lakini watajiunga nasi wakati ufaao,” Naibu Gavana wa Machakoos Francis Mwangangi alinukuliwa akisema majuzi.
Wachanganuzi wanasema wabunge wamegundua kuwa uhasama mashinani unazidi kwa viongozi walioko serikalini, jambo linalowalazimu kutathmini upya mustakabali wao wa kisiasa.
Dkt Gichuki na Bw Mwangangi wanabashiri kuwa hali kama ya mwaka wa 2022 ambapo takriban wabunge 225 kati ya 290 walipoteza viti vyao, huenda ikajirudia mwaka 2027.
Katika Magharibi mwa Kenya, wabunge wameeleza hofu yao kuhusu kile wanachokiita upendeleo katika utekelezaji wa maendeleo, huku wakidai kuwa eneo la Nyanza ambalo kihistoria huunga mkono kiongozi wa upinzani Raila Odinga linapendelewa kuliko kaunti za Magharibi.
“Imekuwa vigumu kuwaeleza watu wetu kwa nini maeneo mengine ambayo hayakuunga mkono serikali hii yanazawadiwa, ilhali sisi tunatengwa. Wafuasi wetu si wajinga, wamesema wazi hawatamuunga mkono Ruto tena mwaka 2027 kama mambo hayatabadilika,” alisema Seneta wa Kakamega Dkt Boni Khalwale.
Kulingana na Mbunge wa Saboti Caleb Amisi, mambo hayatakuwa rahisi kwa Rais Ruto katika eneo la Magharibi mwaka 2027.
“Nimezunguka sehemu nyingi za Magharibi, na nahisi hatari kwa Ruto. Upinzani uko wazi. Baadhi ya viongozi wanaomsifu hadharani wanatengeneza mipango mbadala kwa siri, msishangae kuwaona wakimwacha dakika ya mwisho,” anasema Amisi.
Masaibu ya wabunge yanazidi kuongezwa na wimbi la maandamano ya vijana yaliyoanza mwaka jana dhidi ya serikali.
“Vijana ndio watakuwa wapigakura wengi katika uchaguzi mkuu wa 2027 na wamekuwa wazi kwa chuki yao kwa wabunge wanaounga serikali,” asema Dkt Gichuki.