Habari za Kaunti

Sumu la penzi: Afisa wa KWS aua baunsa na kujiua

Na STANLEY NGOTHO August 18th, 2024 1 min read

MAAFISA wa upelelezi katika eneo la Ong’ata Rongai, Kaunti Ndogo ya Kajiado Kaskazini, wanachunguza kisa  ambapo askari wa Shirika la Huduma ya Wanyamapori (KWS) alimpiga risasi na kumuua mlinzi wa klabu ya usiku na baadaye kujifyatulia risasi  katika mzozo na mwanamke mmoja asubuhi ya Jumamosi.

Kamanda wa Polisi wa Kaunti Ndogo ya Kajiado Magharibi  Ephantus Kariuki, anayemshikilia mwenzake wa Kajiado Kaskazini Bw Hussein Gura ambaye anahudhuria mafunzo rasmi, alithibitisha tukio hili

Aliambia Taifa Jumapili kuwa mshukiwa alikuwa katika baa kando ya Barabara ya Magadi ugomvi ulipotokea kati yake na mwanamume mwingine mwendo wa saa nane mchana siku ya Ijumaa na kumfanya aondoke akiwa na hasira.

Kulingana na ripoti ya polisi, mshukiwa huyo alirejea kwenye baa hiyo mwendo wa saa mbili asubuhi akiwa na bunduki na kuwaamuru watu wengi waliokuwa wakisherehekea kulala chini.

Baadaye akampiga risasi mwanamume  huyo na kumuua papo hapo na akaondoka kwa pikipiki hadi nyumbani kwake alipojiua kwa kujipiga risasi.

“Baada ya kumuua mwathiriwa, aliondoka katika klabu hiyo kwa pikipiki. Tumeanzisha uchunguzi na watu kadhaa walioshuhudia wamenakili taarifa,” alisema Bw Kariuki bila kutoa maelezo zaidi.