• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 11:42 PM
Alexis Sanchez afunga mabao mawili na kusaidia mabingwa Inter Milan kukomoa Sampdoria 5-1 katika Serie A

Alexis Sanchez afunga mabao mawili na kusaidia mabingwa Inter Milan kukomoa Sampdoria 5-1 katika Serie A

Na MASHIRIKA

FOWADI wa zamani wa Manchester United na Arsenal, Alexis Sanchez, alifunga mabao mawili na kuongoza mabingwa wapya wa Ligi Kuu ya Italia (Serie A), Inter Milan, kuwaponda Sampdoria 5-1 mnamo Jumamosi.

Katika mchuano huo uliokuwa wao wa kwanza tangu watwae taji la Serie A kwa mara ya kwanza baada ya miaka 11, Inter wanaotiwa makali na kocha Antonio Conte, walijipata wakiwa kifua mbele kwa mabao 3-1 kufikia mwisho wa kipindi cha kwanza.

Roberto Gagliardini alifungulia Inter ukurasa wa mabao katika ya nne kabla ya Sanchez kucheka na nyavu za wageni wao chini ya sekunde 600 kunako dakika ya 26 na 36.

Andrea Pinamonti alipachika wavuni goli la nne la Inter kunako dakika ya 61 kabla ya Lautaro Martinez kufunga penalti dakika tisa baadaye.

Sampdoria, waliofutiwa machozi na fowadi matata raia wa Senegal, Keita Balde, katika dakika ya 35, sasa wanashikilia nafasi ya tisa jedwalini kwa alama 45 huku zikiwa zimesalia mechi tatu pekee kwa kampeni za muhula huu kutamatika rasmi.

Inter wanajivunia alama 85 huku pengo la pointi 15 likiwatenganisha na nambari mbili Napoli waliowapepeta Spezia 4-1.

MATOKEO YA SERIE A (Jumamosi):

Inter Milan 5-1 Sampdoria

Spezia 1-4 Napoli

Udinese 1-1 Bologna

Fiorentina 2-0 Lazio

You can share this post!

Neymar sasa kuchezea PSG hadi 2025

Mahangaiko tele, wakazi Juja Farm walazimika kukarabati...