Na MASHIRIKA
MABINGWA watetezi Brazil wako pazuri kuhifadhi dhahabu ya Olimpiki mwaka huu baada ya kudengua Mexico kwa penalti 4-1 kwenye hatua ya nusu-fainali.
Mshindi wa mechi hiyo iliyochezewa uwanjani Kashima, Japan aliamuliwa kupitia penalti baada ya pande zote mbili kusajili sare tasa kufikia mwisho wa muda wa ziada.
Kipa wa Brazil alipangua penalti ya Eaduarso Aguirre kabla ya Johan Vasquez wa Mexico kushuhudia kombora lake likigonga mhimili wa goli la Brazil.
Brazil watakutana sasa na Uhispania kwenye fainali ambayo itafanyika Agosti 7, 2021.
Dani Alves, Bruno Guimaraes, Reinier na Gabriel Martinelli wa Arsenal wote walifunga penalti zao kwa upande wa Brazil.
Mshindi wa nusu-fainali ya pili kati ya Uhispania na wenyeji Japan nusura pia aamuliwe kupitia penalti. Hata hivyo, Marco Asensio wa Real Madrid alifungia Uhispania bao la pekee na la ushindi katika dakika ya 115 uwanjani Saitama.
Asensio alitokea benchi katika kipindi cha pili na kuongoza Uhispania kutinga fainali ya kwanza ya Olimpiki tangu waambulie nafasi ya pili kwenye michezo iliyoandaliwa jijini Sydney, Australia mnamo 2000.
TAFSIRI NA: CHRIS ADUNGO