• Nairobi
  • Last Updated March 29th, 2024 5:46 PM
ERIC MALANDA: Aanzisha timu yenye makali ligini licha ya kuwa mlemavu

ERIC MALANDA: Aanzisha timu yenye makali ligini licha ya kuwa mlemavu

Na PATRICK KILAVUKA

UTU na ari ya Eric Malanda imemwezesha kuanzisha timu ya Tinganga Community FC, Kaunti ya Kiambu ambayo inatia fora ligini japo yeye mlemavu. Isitoshe, anamini kwamba wema hauozi kwa kuchochea na kukuza vipaji vya soka mtaani.

Muasisi Malanda anasema kiu ya kutandaza boli kilimsakama akiwa bado angali mdogo lakini ulemavu ukakikatiza.

Aliamua kufikiria kwa kina na kuwa na mtazamo chanya mwaka wa 2016 kuhusu kutimiza ndoto yake ya kusakata boli kisha akaamua kustawisha timu ambayo atakuwa anaitolea mawaidha na ushauri nasaha kuijenga zaidi katika ulimwengu wa kabumbu.

“Sikuwa na kosekana uwanjani haswa timu ya mtaani ya Tinganga United ilikuwa inacheza kwa minajili ya kuishabikia japo miye mlemavu. Lakini niliamini soka inaweza kuchezwa kiakili na hapo ndipo niliibua wazo la kuwa na timu,” asema muasisi huyo ambaye pia ni meneja wa timu hii ambayo ilifungua milango miaka miwili iliyotuga.

Timu hii chini ya usimamizi wake, inapigia mechi zake na kujinolea katika uga wa Tinganga/ Kamunyonge Stadium, Kiambu.

Tinganga United yaondoka uwanjani baada ya mazoezi huku kinara wao (mwenye kigari cha walemavu) akiwapa maelekezo. Picha/ Patrick Kilavuka

Ina wanasoka 30. Aliianza tu na wachezaji watano ambao aliwavua baada ya kuwaelezea nia yake ya kutosa ndaono kwao kustawisha timu na wakaitikia wito huo.

“Nilitoa hawa vijana katika uraibu wa ulevi na nikawashawishi kucheza boli kwani ninauthamini mchezo huu licha ya hali yangu. Isitoshe, niliwaambia kwamba, ningependa kuirudishia jamii mkono kupitia kukuza vipaji vya soka. Fauka ya hayo, nilipenda kuona vipawa vya soka vikitumika ipasavyo,” aeleza mraibu huyo wa soka ambaye alianza timu na wanasoka James Gatho, Brian Kameri, James Waweru, Josphat Mwangi na Robert Wahiti.

Kutokana na nia yake njema, timu inazidi kupanuka huku akiwa anasaidiana na kocha George Gitau kuwapokeza malezi ya soka wanakandanda hawa ambao wamekuwa moto wa kuotewa mbali kwani, wanahemesha timu pinzani katika ligi ya Kaunti ya Kiambu.

Eric Malanda (kati) akiwafunza vijana wake mbinu za soka. Picha/ Patrick Kilavuka

Mwaka 2017, walichomoa makucha kwenye ligi ya FKF, Kauntindogo ya Kiambu na kuibuka wa tatu bora baada ya kuzoa alama 54 miongoni mwa timu kumi na tano wakiwa nyuma ya Tinganga United (55) na mabingwa Maria FC (57) na kupewa fursa ya kuendeleza usogora wao katika ligi ya FKF, Kaunti Tawi la Aberdare.

Ni mwaka wao wa kwanza ligini lakini makali yao yamehisiwa kutokana na matokeo ya kufurahisha ambayo inayasajili katika michuano ambayo wamepepeta dhidi Maradona ambapo waliinyorosha 6-0, kuandikisha sare ya 2-2 katika mechi yao dhidi ya TCM na Destiny FC, sare zingine mbili za 1-1 dhidi ya TNT na Mwimuto Wailers Jr uwanjani Approved, Lower Kabete na hatimaye, kupoteza moja dhidi ya Nyamathombi kwa kucharazwa 2-1.

Kuifumbatia timu, uthamini wa kila mchezaji, kuweka kando ukabila na kuzingatia nidhamu kama silaha yao na mashabiki wengi kujitokeza kushabikia zaidi katika kila mechi, uvuvuo wa talanta mtaani na matokeo bora yanaonekana.

Fauka ya hayo, dukuduku ambalo lilikuwa ndani mwa wengi wakati alipokuwa anaianzisha eti hatafua dafu, liliyeyuka baada ya timu kuvuka daraja ya ligi ya Kauntindogo ya Kiambu kwa matao na kuanza kukita mizizi katika ligi ya Kaunti.

Vijana wa Tinganga United wakiwa mazoezini. Picha/ Patrick Kilavuka

Pia, wanajamii wameanza kuisaidia kuimarika zaidi.

“Changamoto ambayo nimekuwa nayo ni kwamba wanajamii mwanzoni hawakubali kwamba, ninaweza kuidumisha lakini baada ya kungangana nayo katika ligi ya Kauntindogo na kupata matokeo ya kuridhisha, wahisani katika jamii ya Tinganga wameona umaana wa timu kuwepo katika kulea vipawa vya soka na wameniunga mkono ili, ndoto ya vijana kucheza soka tamanifu itimie.

Kando na hayo kujitolea kwa wachezaji kikamilifu, kunanipa motisha ya kuwatia moyo zaidi kwa kuwekeza pato langu japo ndogo katika kuikuza timu na hivyo ndivyo tumekuwa tukiendeleza kampeni yetu katika ligi,” aeleza Malanda ambaye ni muuzaji viazi mjini Kiambu na ni shabiki sugu wa timu ya Chelsea.

Ili kuendelea kuvuta ya kamba ya timu, mwanzilishi huyo anajaribu kuongea na viongozi wa eneo hilo kuhusu kuihisani timu, lakini hajapata jibu la kuridhisha ila, angeomba wahisani kujitokeza kwa hali na mali kuisaidia kuinua vipawa.

Mipango? Ni wacheza sasa katika ligi ya Kanda ya Mkoa wa Kati mwakani na kulenga ligi kuu nchini majaliwa. Anaamini kwamba wakiwa na umoja na mshikamano wa mnato zaidi, wataweza!

You can share this post!

KONOKONO: Ngonjera inayotetea haki za mtoto wa kiume

Timu ya Kamukunji inavyokuza vipaji mitaani

adminleo