• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 11:42 PM
Inshallah nchi yetu iwe na amani zaidi mwaka 2022

Inshallah nchi yetu iwe na amani zaidi mwaka 2022

Na WALLAH BIN WALLAH

KWANZA kabisa tumshukuru Mwenyezi Mungu kwa rehema zake za kuwa nasi tangu mwanzo wa mwaka 2021 hadi tukafika tulipofika leo.

Jina lake lihimidiwe!

Pili tuwaombee wenzetu tulioanza nao safari pamoja lakini kwa mapenzi ya Mola Muumba wetu wakaitikia wito usiopingika! Roho zao zihifadhiwe mahali pema peponi! Amina!

Safari ya maisha ni kupanda na kushuka. Ni mwendo wa kuelekea mbele bila kujua mwisho ni lini! Sisi tuliofika tulipofika leo hatuna chochote cha kujivunia kwa sababu ni kudra zake Mungu tu! Siyo kwa sababu ya uwezo wetu wala ubora wetu! La hasha!

Kwa mintaarafu hiyo, nitumie muda huu kuwakumbusha wananchi wenzetu kwamba mihemko na makeke makeke ya midomo midomo ya jazba za kampeni za uchaguzi wa mwaka ujao 2022 visiwafanye kusahau thamani ya uhai! Hasa nyinyi wanasiasa onesheni mfano bora! Kuweni waadilifu hata kama hamwezi kuwa watakatifu!

Chagueni maneno ya kuyasema ili kuepuka shari! Siasa siyo mapambano ya vita na mabavu! Siasa ni sayansi ya kulumbana kwa kutumia busara na hekima kuuza sera! Siasa siyo maabara ya kufanyia majaribio ya ubabe, ujeuri, upana wa kifua na umiliki wa mali!

Siasa siyo ufundi wa kutoa kashfa na matusi. Ni umahiri wa kufafanua sera na uongozi bora! Kama huna sera tia mdomo kufuli! Usitumie demokrasia vibaya! Sharti tujue tofauti kati ya Demokrasia na Demoghasia! Chonde chonde! Tunataka amani zaidi mwaka 2022!!!!

  • Tags

You can share this post!

Mtiririko wa vitushi, wahusika na maudhui Sura ya 7 –...

NBC: Chama cha Uanahabari katika shule ya Upili ya Ndalani,...

T L