• Nairobi
  • Last Updated April 23rd, 2024 10:55 AM
TAHARIRI: IPOA ilikosa kuafikia matarajio ya wengi

TAHARIRI: IPOA ilikosa kuafikia matarajio ya wengi

Na MHARIRI

Bodi ya Mamlaka ya Usimamizi wa Huduma za Polisi ilimaliza hatamu yake Jumatatu ikiwa imekamilisha uchunguzi wa kesi 752 kati ya 9,248 zilizofikishwa kwenye meza yao.

Kulingana na ripoti yao ya mwisho, visa vya utumizi mbaya wa mamlaka vilichukua asili mia 45.1 ya kesi zote zilizoripotiwa huku asili mia iliyobakia ikiwa ni visa kuhusu unyanyasaji unaofanywa na maafisa wa polisi, mauaji ya kiholela na dhuluma za kimapenzi zinazofanywa na maafisa wa usalama.

Kwa kuangalia utendakazi mzima wa bodi hiyo kwa jumla, unaweza kuhisi kwamba haikuafikia matarajio makubwa Wakenya waliokuwa nayo kwa taasisi kama hiyo.

Kufaulu kuhukumu polisi kwa makosa katika visa vitatu pekee katika kipindi cha miaka sita, ni mzaha mkubwa mbali na kuwa kinaya kikuu katika taifa linalosema linafuata sheria.

Ni siri iliyo wazi kwamba katika taifa hili, kitengo cha polisi kiko miongoni mwa taasisi zinazohusishwa na hujuma, dhuluma, mauaji, utepetevu na ukandamizaji wa haki za kimsingi za kibinadamu.

Na kama kunaye anayehitaji mfano mzuri wa jinsi idara ya polisi inavyokandamiza haki za kimsingi za binadamu, basi anahitaji kusoma habari za mauaji ya mwanamke katika Bustani ya City, Nairobi, wikendi iliyopita.

Bi Janet Waiyaki, mama wa watoto watatu wachanga, alimiminiwa risasi na kuuawa akiwa kwenye gari na mwanamume mmoja, ambaye baadaye alifahamika kuwa jamaa yake, Bw Bernard Chege.

Polisi wanasema walishuku wawili hao walikuwa wahalifu waliokuwa ‘katika mazingira ya kutatanisha’ kwa jinsi walivyokosa kufungua dirisha la gari walipotakiwa kufanya hivyo.

Lakini familia inashangaa jinsi maafisa hao wa polisi kutoka Makadara, walivyomiminia gari hilo zaidi ya risasi 15 bila kuwa na ushahidi kwamba wawili hao walikuwa wahalifu.

Kisa hiki kingelikuwa muhimu kwa bodi ya IPOA kuthibitisha umuhimu wa kuweko kazini wakilipwa kitita cha pesa na mlipa ushuru, lakini kwa bodi iliyoshindwa kutoa majibu kuhusu mauaji ya Mtoto Pendo mjini Kisumu, mwaka 2017, pamoja na kuuawa kwa risasi kwa watoto Stephanie Moraa na Geoffrey Mutinda waliokuwa wanacheza nyumbani kwao wakati wa patashika katika ya wafuasi wa NASA na polisi Nairobi, kwa kweli ilikuwa vigumu kutarajia lolote la tija kutoka kwao.

 

You can share this post!

Weita mpenda ombaomba amwaga unga

WANDERI: Waafrika wangali watumwa wa Wazungu

adminleo