• Nairobi
  • Last Updated April 18th, 2024 9:55 AM
#JkuatLivesMatter: Majina ya polisi katili yatolewa

#JkuatLivesMatter: Majina ya polisi katili yatolewa

NA MARY WANGARI

KISA cha mwanafunzi wa Chuo Kikuu cha Jomo Kenyatta (JKUAT) aliyepigwa kikatili na polisi kimechukua mkondo mpya huku Mamlaka Huru ya Uangalizi (IPOA) ikiwatambua maafisa wote 50 waliohusika na oparesheni hiyo na baadhi ya majina ya maafisa hao kutangazwa.

Haya yamejiri huku Tume ya Kitaifa kuhusu Huduma ya Polisi (NSPC) hatimaye ikitaja majina ya maafisa wanne walioibua hasira nchini na kimataifa waliponaswa kwenye video iliyosambazwa mno mitandaoni, wakimpiga kinyama mwanafunzi ambaye hakuwa amejihami.

Akihutubia wanahabari jana, Mwenyekiti wa NSPC Bw Eliud Kinuthia aliwatambulisha maafisa hao kama Koplo George Wathania, Makonstebo wa Polisi Jonathan Kibet na Boniface Muthama.

Bw Kinuthia alisema kuwa afisa wa nne alikuwa bado hajatambuliwa na kufafanua kuwa Msimamizi wa Kituo cha Polisi cha Thika, Koplo Mathew Masaga aliyeongoza oparesheni hiyo, alikuwa miongoni mwa waliojeruhiwa katika kisa hicho.

Kulingana na taarifa ya Tume ya Kungazia Utendakazi wa Polisi (IPOA) iliyotiwa sahihi na Mwenyekiti, Anne Makori, maafisa hao wanne wamesimamishwa kazi huku uchunguzi kuhusu kisa hicho ukiendela.

Ripoti hiyo ilisema kuwa wanafunzi wasiopungua 22 walijeruhiwa wakati wa kisa hicho.

“IPOA imewasiliana na kuchukua taarifa kutoka kwa walioshuhudia kisa hicho. Kutokana na ripoti hii, mamlaka sasa imeanza uchunguzi kamili kuhusu tukio hilo,” akasema Bi Makori.

Haya yamejiri siku moja tu baada ya Inspekta Jenerali wa Polisi, Hilary Mutyambai kutoa amri ya kuwakamata maafisa hao walionaswa katika videoya kisa hicho.

Mnamo Jumanne, Wakenya pamoja na mashirika mbalimbali ya kutetea haki za kibinadamu walijitosa mitandaoni kuelezea hasira zao kuhusu kisa hicho cha kushtusha ambapo maafisa wanne wa polisi walinaswa wakimpiga kinyama mwanafunzi.

Tukio hilo lilijiri wanafunzi wa JKUAT walipokuwa wakishiriki maandamano ya amani nje ya chuo hicho wakilalamikia ukosefu wa usalama chuoni humo.

You can share this post!

‘Mzee Moi anaendelea vyema hospitalini’

AFLATOXIN: Amri wauzaji waondoe unga hatari madukani

adminleo