Na GEOFFREY ANENE
KAMATI Kuu ya timu ya Olimpiki ya Kenya inataka serikali iwape wanamichezo watakaowakilisha taifa kwenye Olimpiki kipaaumbele katika utoaji wa chanjo ya virusi vya corona.
Ilieleza Alhamisi kuwa wanamichezo wanasafiri nje ya nchi mara kwa mara kwa shughuli ya mazoezi na mashindano.
Kamati hiyo ya watu 39 pia ilifichua kuwa zoezi la kupima wanamichezo ugonjwa wa covid-19 unaosababishwa na virusi hivyo, limefanya bajeti ya Olimpiki kuongezeka.
“Mbali na kupima wanamichezo mara kwa mara wanapoenda kushiriki mashindano ya kufuzu, kila mtu atahitajika kupimwa saa 72 kabla ya kuelekea mjini Tokyo nchini Japan, mara anapowasili, kila baada ya siku nne wakati wa mashindano na kabla ya kurejea nyumbani,” kamati hiyo ilisema baada ya kikao chake cha kwanza Alhamisi tangu ichapishwe rasmi tena katika gazeti la serikali Februari 12.
Kamati hiyo inayoongozwa na naibu rais wa kwanza wa Kamati ya Kitaifa ya Olimpiki Kenya (NOC-K) Shadrack Maluki ilipokea ripoti kuhusu maandalizi ya Kenya kutoka kwa Kiongozi wa msafara Waithaka Kioni.