Na WANGU KANURI
SENETA maalum Karen Nyamu ameeleza hofu yake baada ya bingwa wa dunia na mshikilizi wa rekodi ya dunia katika marathon, Eliud Kipchoge kushindwa katika mbio za Jumatatu za Boston.
Kipchoge alimaliza wa sita katika riadha hiyo kwa saa 2 dakika 09 na sekunde 23, baada ya Evans Chebet ambaye aliongoza kwa saa mbili dakika 05 na sekunde 54.
“Ni nini kinafanyika kwa bingwa wetu? Ni wakati wake kuondoka sasa ili tumkumbuke kwa ushindi na tusihudhurie siku kama hizi?” akauliza.
Licha ya kushindwa katika riadha ya Jumatatu, Kipchoge alieleza kuwa katika michezo yoyote kuna wakati wa kushinda na kushindwa.
“Ninafurahia nyakati ambazo ninaweza kupita mipaka. Si hakika mtu atafaulu kwani si rahisi. Leo haikuwa rahisi. Niling’ang’ana niwezavyo lakini nyakati zingine, lazima tuelewane kuwa leo haikuwa siku ya kupita mipaka na kuweka rekodi mpya,” akasema kupitia ukurasa wake wa Twitter.
Mwaka wa 2020, Kipchoge alimaliza wa nane katika London Marathon kwa 2:06:49 zaidi ya dakika moja nyuma ya mshindi Shura Kitata wa Ethiopia.
Bingwa huyu atahitajika kushindana kwa riadha zingine mbili kabla ya Paris Games.
Licha ya kushindwa katika Boston Marathon 2023, hakuna aliyeweza kuivunja rekodi aliyoweka mwaka jana ya 2:01:09.
Aliyekuwa karibu sana kuvunja rekodi hiyo alikuwa Geoffrey Mutai kwa dakika 2:03:03 mwaka wa 2011.
Kipchoge ameweza kuzawadiwa tuzo kadha wa kadha katika maisha yake ya uanariadha huku akiibuka mwanariadha bora duniani mwaka 2018 na 2019.