NA JESSE CHENGE
GAVANA wa Bungoma Kenneth Lusaka amewasihi viongozi waliochaguliwa katika kaunti hiyo kuzingatia majukumu yao na kumruhusu kutimiza ahadi zake kwa wananchi.
Bw Lusaka anasema ni jukumu lake kuhakikisha ameafikia sera na miradi ya maendeleo aliyoahidi wakati akiomba kura kuchaguliwa Agosti 2022 kuwa Gavana.
Lusaka alielezea wasiwasi kuhusu mgongano wa kisiasa Bungoma, akihoji mkondo ambao baadhi ya wanasiasa wamechukua huenda ukalemaza jitihada zake.
“Tulichaguliwa pamoja ili kutumikia kwenye nafasi tofauti. Kila mmoja wetu anapaswa kuzingatia majukumu yake kikamilifu,” Bw Lusaka alisema.
Gavana alitoa malalamishi kutokana na siasa zinazozingira Bodi ya Huduma kwa Umma katika Kaunti, akisema Katiba imeipa mamlaka kuteua watu kwa msingi wa uwezo wao, na kwa hiyo, haipaswi kuingiliwa.
“Acheni Bodi ya Huduma kwa Umma itimize majukumu yake kuteua Katibu wa Kaunti na kutupatia mgombea anayefaa. Msiingilie mchakato huo,” Bw Lusaka alisisitiza.
Alitoa kauli hiyo Jumatatu, Oktoba 9, 2023 wakati wa
hafla ya kuapishwa kwa wajumbe wa Bodi ya Manispaa katika, Makao Makuu ya Kaunti ya Bungoma.