• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 9:35 PM
Kicheko bungeni abiria wanaochafua hewa kwa ndege wakijadiliwa

Kicheko bungeni abiria wanaochafua hewa kwa ndege wakijadiliwa

Na CHARLES WASONGA

MBUNGE wa Rangwe Lilian Gogo  (pichani) aliibua kicheko bungeni Jumatano alasiri alipopendekeza kuwa abiria wa ndege wenye matatizo ya tumbo wapewe tembe za kupunguza asidi ili kuwazuia kutoa hewa mbaya (kunyamba) ambayo husababisha usumbufu kwa abiria wengine.

Akichangia mjadala kuhusu Sheria ya Kudhibiti Makosa ambayo hutendwa na abiria kwenye ndege, Bi Gogo alisema kunyamba katika ndege ni usumbufu ambao mara nyingi hupuuzwa.

“Kando na masuala mengine ambayo yanaweza kuhatarisha usalama au kusababisha usumbufu kwa abiria, mnyambo pia ni chanzo cha usumbufu japo hupuuzwa. Kuna abiria ambao hutoa harufu inayokera zaidi baada ya kunyamba,” akasema Bi Gogo.

Mbunge huyo aliongeza kuwa mnyambo pia husababisha machungu kwa abiria wanaosafiri kwa ndege.

“Kunapasa kuwa na sheria inayodhibiti chakula kinachopewa abiria katika ndege kando na mikakati ya tiba ambayo inaweza kupunguza kiwango cha gesi mbaya ambayo mtu anaweza kutoa kwenye ndege,” Bw Gogo akalalamika.

Mbunge huyo alitoa mifano ndege ambazo husafiri kutoka Kisumu kwenda Nairobi akisema ndiko abiria hunyamba kila mara bila kujizuia.

“Hii ndio maana napendekeza kuwa mashirika ya ndege yanayohudumu katika ruti hiyo yawape abiri dawa za kupunguza aside ili kuzuia kero hili,” Dkt Gogo akakariri.

“Sheria iwepo ya kuwazilazimisha mashirika ya ndege kununua dawa kama vile Eno na kuwapa abiria wao ambao huenda wakapata matatizo ya tumbo kwa kula chakula nyingi kupita kiasi,” akaongeza.

Spika wa muda Chris Omulele aliunga mkono pendekezo la Dkt Gogo alisema tabia ya abiria kunyamba imekithiri zaidi katika baadhi ya abiria hulazimika kuvumilia usumbufu wakiwa safarini.

Dkt Gogo pia anapendekeza sheria kuanzishwa na mashirika ya ndege kwa ajili ya kudhibiti kiwango cha pombe ambayo hupewa abiria.

Alisema baadhi ya abiria ambao hudhihirisha tabia mbaya katika ndege wamebainika kuwa walevi baada ya kubugia pombe kupita kiasi.

“Mbona sheria ya kudhibiti kiwango cha pombe ambayo inaruhusiwa kunywewa na abiria kwani baadhi yao hunywa pombe nyingi wanayopewa?

Wabunge waliochangia mjadala huo walisema mabadiliko yanapasa kufanywa na jumuiya ya mataifa kuhusu usalama wa abiria katika ndege, ikiwemo kuimarishwa kwa mafunzo yanayotolewa kwa wahudumu wa ndege.

“Wanafa kufunzwa mbinu bora za kuwadhibiti abiria wanaonyesha mienendo mibaya safarini,” akasema Mbunge wa Kimilili Chris Wamalwa.

Alisema wahudumu wanapasa kufunzwa kwamba abiria hawafai kuruhusiwa kubugia pombe kupita kiasi,” akasema.

You can share this post!

Sh1000: Tuwakumbushe mama na nyanya zetu mashambani kuhusu...

Waiguru, Aukot wakwaruzana tena kuhusu Punguza Mizigo

adminleo