• Nairobi
  • Last Updated April 24th, 2024 10:08 PM
Kipa Aaron Ramsdale aitwa kambini mwa Uingereza kuwa kizibo cha Dean Henderson aliyepata jeraha

Kipa Aaron Ramsdale aitwa kambini mwa Uingereza kuwa kizibo cha Dean Henderson aliyepata jeraha

Na MASHIRIKA

KIPA Aaron Ramsdale wa Sheffield United ameitwa katika timu ya taifa ya Uingereza inayoshiriki fainali za Euro kujaza nafasi ya Dean Henderson anayeuguza jeraha.

Henderson ambaye ni mlinda-lango wa Manchester United, ameondolewa kwenye orodha ya wanasoka watakaotegemewa na kocha Gareth Southgate kwenye mapambano ya Euro 2020 baada ya kupata jeraha la paja mazoezini.

Jeraha hilo litamweka nje kwa kipindi kirefu na tayari amerejea uwanjani Old Trafford kwa matibabu zaidi.

“Nilijitahidi sana kuitwa kambini mwa Uingereza. Inasikitisha kwamba sasa imenilazimu kujiondoa kambini kwa sababu ya jeraha. Nawatakia wanasoka wenzangu kila la heri katika mechi zijazo na nina matumaini tele kwamba watatawazwa mabingwa wa Euro mwaka huu,” akaandika Ramsdale kwenye mtandao wake wa Twitter.

Ingawa Ramsdale, 23, hajawahi kuchezea Uingereza katika mchuano wowote, alitiwa na Southgate kwenye kikosi cha awali cha wachezaji 33 kwa ajili ya fainali za Euro.

Ramsdale sasa ni miongoni mwa makipa watatu wanaojivuniwa na Uingereza kambini mwao kwa ajili ya kipute cha Euro mwaka huu. Anaungana na Jordan Pickford wa Everton na Sam Johnstone wa West Bromwich Albion.

Uingereza walifungua kampeni zao za Kundi D kwenye Euro kwa ushindi mwembamba wa 1-0 dhidi ya Croatia mnamo Juni 13 ugani Wembley, London. Watapepetana na Scotland katika mechi yao ya pili mnamo Juni 18, 2021 uwanjani Wembley.

Mbali na Henderson, mchezaji mwingine ambaye amepata jeraha katika kambi ya mazoezi ya Uingereza ni beki wa kushoto wa Man-United, Luke Shaw. Nafasi yake itatwaliwa sasa na Kieran Trippier wa Atletico Madrid au Ben Chilwell wa Chelsea.

TAFSIRI NA: CHRIS ADUNGO

You can share this post!

Huduma za choo, bafu zarejelewa eneo la Crescent baada ya...

Pwani kuwa na madereva 4 Safari Rally