• Nairobi
  • Last Updated April 25th, 2024 8:55 PM
Kisumu All Stars kutaja benchi mpya ya kiufundi

Kisumu All Stars kutaja benchi mpya ya kiufundi

Na CHRIS ADUNGO

KIKOSI cha Kisumu All Stars kitafichua benchi mpya kiufundi baada ya mchujo wa mikondo miwili dhidi ya Vihiga United.

Mechi hizo zitalenga kubaini klabu ya ziada itakayoshuka daraja kwenye Ligi Kuu ya FKFPL msimu ujao na kitakachopanda ngazi kutoka NSL kwa minajili ya kinyang’anyiro cha muhula mpya wa 2020-21.

Mechi ya mkondo wa kwanza itasakatwa mnamo Oktoba 7 na marudiano kuandaliwa Oktoba 11, 2020. Kisumu All-Stars walishikilia nafasi ya 16 kwenye jedwali la vikosi 18 vya KPL mnamo 2019-20 huku Vihiga United wakimaliza kampeni za NSL katika nafasi ya tatu nyuma ya Bidco United na Nairobi City Stars waliokwezwa daraja kunogesha Ligi Kuu msimu ujao wa 2020-21.

“Tulipokea idadi nzuri ya barua za maombi kutoka kwa wakufunzi wazawa wa humu nchini na wengine kutoka mataifa ya nje. Bodi ya Usimamizi ya All Stars inapitia barua hizo kabla ya kuwatathmini walioziwasilisha kisha kufichua benchi mpya baada ya mikondo miwili ya mchujo dhidi ya Vihiga,” akasema Nicholas Ochieng ambaye ni Afisa Mkuu Mtendaji wa All Stars.

All Stars almaarufu ‘Blue Eagles’ wanadhaminiwa na Serikali ya Kaunti ya Kisumu. Mbali na kocha mkuu, kikosi hicho kinasaka kocha msaidizi, kocha wa viungo vya mwili na kocha wa makipa.

Ochieng amesema kwamba tayari wameanza maandalizi kwa minajili ya mchujo ujao na wanasoka wake wana matumaini ya kuibuka washindi na kuhifadhi nafasi yao kwenye Ligi Kuu ya KPL msimu ujao.

“Ingawa wanasoka wetu wamekuwa katika likizo ndefu tangu ujio wa corona, kila mmoja wao amekuwa akishiriki mazoezi kivyake. Tutatumia wiki hizi tatu zijazo kujiandaa vilivyo kwa kibarua kilichopo mbele yetu na tuna kila sababu ya kushinda,” akaeleza Ochieng.

Kwa mujibu wa Frank Ogolla ambaye ni Mkuu wa Mashindano katika Shirikisho la Soka la Kenya (FKF), mkutano utaandaliwa wiki hii ili kupata mwafaka kuhusu kikosi kitakachocheza nyumbani katika mkondo wa kwanza ili kiwe ugenini wakati wa marudiano.

Vihiga United wanalenga pia kurejea kwenye KPL baada ya kuambulia nafasi ya tatu kwenye NSL. All Stars kwa upande wao wanapania kuendelea kuwa wawakilishi wa eneo la Nyanza kwenye kampeni za Ligi Kuu muhula ujao.

Kuteremshwa ngazi kwa wanasukari wa Chemelil Sugar na SoNy Sugar kunasaza All Stars pekee na Western Stima wakiwa wawakilishi wa eneo la Nyanza kwenye KPL.

Kufikia sasa, Stima wameagana na wanasoka 11 tangu kampuni ya umeme ya Kenya Power iliyokuwa ikiwadhamini isitishe ufadhili. Wengi wa wachezaji hao waliobanduka Stima wamesajiliwa na Wazito FC na mabingwa mara 19 wa KPL, Gor Mahia. Aliyekuwa mkufunzi mkuu wa Stima pia, Salim Babu aliyoyomea Wazito kuwa kocha msaidizi.

Mnamo Agosti, All Stars walitangaza nafasi za kazi katika benchi yao nzima ya kiufundi.

“Bado hatujapata kocha mpya lakini tutamtegemea Andrew Aroka atuongoze katika mechi mbili zijazo dhidi ya Vihiga United. Amekuwa na kikosi kwa muda mrefu na miongoni mwa wakufunzi ambao wametuma maombi ya kupokezwa kazi ya ukocha,” akasema Ochieng.

All Stars waliagana rasmi na Jeff Odongo (kocha wa viungo vya mwili) na Fredrick Onyango (kocha wa makipa) walioteuliwa kuhudumu katika benchi ya kiufundi mnamo Februari 2020.

Aroka ndiye afisa aliyewahi kuhudumu kambini mwa kikosi hicho kinachodhaminiwa na Serikali ya Kaunti ya Kisumu kwa muda mrefu zaidi na ndiye aliyechangia kupandishwa ngazi kwa kikosi hicho kushiriki soka ya Ligi Kuu mwanzoni mwa msimu huu wa 2019-20.

Mnamo Januari 2020, All Stars walimtimua aliyekuwa kocha wao wa muda mrefu, marehemu Henry Omino kwa pamoja na aliyekuwa msaidizi wake, Aroka na kocha wa makipa Joseph Ongoro kwa sababu ya matokeo duni ya kikosi.

Hata hivyo, Aroka alirejea baadaye kambini mwa klabu hiyo baada ya Arthur Opiyo aliyeteuliwa kushikilia mikoba ya kikosi hicho kwa muda kurejea Ujerumani kwa mafunzo zaidi ya ukocha.

Mbali na Aroka, wengine ambao wametuma upya maombi ya kazi kambini mwa All Stars ni Odongo na Onyango.

“Walikuwa wametia saini mikataba ya miezi michache ambayo kwa sasa imekatika. Wamewasilisha upya maombi ya kazi kwa minajili ya kuendelea kuhudumu nasi katika benchi mpya ya kiufundi ambayo tunapania kuifichua rasmi mwishoni mwa Septemba,” akasema Ochieng kwa kusisitiza kwamba wanamtafuta kocha mkuu aliye na leseni ya kiwango cha C kutoka kwa Shirikisho la Soka la Afrika (CAF).

  • Tags

You can share this post!

Kaunti zote zitapokea fedha Jumatatu – Serikali

Waliotafuna mamilioni ya corona kujua hatima yao baada ya...