• Nairobi
  • Last Updated March 29th, 2024 12:58 PM
Kituyi akemea Uhuru, amtaja kama dikteta

Kituyi akemea Uhuru, amtaja kama dikteta

Na Brian Ojamaa

WAZIRI wa zamani na mwaniaji wa urais hapo mwakani, Dkt Mukhisa Kituyi amekashifu utawala wa Rais Uhuru Kenyatta kwa kuwakandamiza wapinzani ambao wanalenga kuwania nyadhifa mbalimbali za uongozi.

Dkt Kituyi wikendi alisema kuwa wanasiasa wanaoonekana kuwa na mtazamo kinzani kuhusu masuala mbalimbali ya uongozi wamekuwa wakinyanyaswa huku serikali ikiwalazimishia raia baadhi ya viongozi.

Akihutubu wakati wa mazishi ya Mzee Charles Wekesa Maruti katika wadi ya Maraka, Webuye Mashariki, Dkt Kituyi alidai kuwa serikali imekuwa ikiwatumia maafisa wa usalama kuwatishia wapinzani wake.

“Wale ambao hawaiungi mkono serikali wamekuwa wakitishiwa kuwa watashtakiwa kortini kutokana na makosa mbalimbali. “Kenya ni nchi yenye demokrasia na kila mmoja ana uhuru wa kuamua mkondo wa kisiasa anaoutaka,” akasema.

Akigusia suala la ufisadi, Katibu huyo wa zamani wa Shirika la Kimataifa la UNACTAD, alisema tofauti za kisiasa hazifai kutumika kuwasawiri baadhi ya viongozi kama wafisadi.

“Ni kinaya kuwa Rais alikuwa ameilamu mahakama kwa kujikokota kukabiliana na kesi za ufisadi ilhali baadhi ya watu wanalazimishwa wabadilishe misimamo yao ya kisiasa,” akaongeza.

Alitoa wito kwa wanasiasa wote waendeleze kampeni ya amani na wajizuie kuwagonganisha Wakenya.

You can share this post!

CECIL ODONGO: Kupe wa kisiasa wataponza Mudavadi na Kalonzo...

Wanasiasa wasukuma vijana wachukue vitambulisho