Na MASHIRIKA
BAYERN Munich walihitaji penalti ya dakika za mwisho kutoka kwa Robert Lewandowski ili kuzamisha Augsburg 1-0 katika Ligi Kuu ya Ujerumani (Bundesliga) mnamo Jumamosi ugani Allianz Arena.
Bayern walishuka dimbani kuvaana na Augsburg siku chache baada ya Villarreal kuwapokeza kichapo cha 1-0 katika mkondo wa kwanza wa robo-fainali ya Klabu Bingwa Ulaya (UEFA).
Licha ya kupigiwa upatu wa kukomoa Augsburg kirahisi, Bayern walitolewa jasho na kikosi hicho kinachokodolea macho hatari ya kuteremshwa ngazi katika Bundesliga muhula huu.
Bao la Lewandowski lilikuwa la 23 kwa nyota huyo raia wa Poland kufunga dhidi ya Augsburg kutokana na mechi 19. Penalti hiyo ilitokana na tukio la Reece Oxford kunawa mpira ndani ya kijisanduku katika dakika ya 82.
Huku Augsburg wakishikilia nafasi ya 14 kwa alama 32, Bayern wanaselelea kileleni mwa jedwali la Bundesliga kwa alama 69, tisa zaidi kuliko nambari mbili Borussia Dortmund.
MATOKEO YA BUNDESLIGA (Jumamosi):
Bayern 1-0 Augsburg
Cologne 3-2 Mainz
Furth 0-2 M’gladbach
Wolfsburg 4-0 Arminia
Hertha Berlin 1-4 Union Berlin
TAFSIRI NA: CHRIS ADUNGO