• Nairobi
  • Last Updated March 29th, 2024 9:50 AM
Mabwanyenye Mlima Kenya wawanunulia polisi magari ya mamilioni

Mabwanyenye Mlima Kenya wawanunulia polisi magari ya mamilioni

Na NICHOLAS KOMU

MABWANYENYE kutoka eneo la Mlima Kenya wakiongozwa na Mwenyekiti wa Benki ya Equity Peter Munga wamenunua magari 26 ya thamani ya Sh100 milioni yatakayotumiwa na maafisa wa utawala katika eneo hilo.

Matano kati ya magari hayo ya kifahari yaliyonunuliwa na Wakfu wa Mlima Kenya yalipokezwa Waziri wa Masuala ya Ndani, Dkt Fred Matiang’i Alhamisi mjini Nyeri.

Magari yaliyosalia yatawasilishwa kwa wizara hiyo baadaye. Bw Munga ambaye ndiye mwenyekiti wa Wakfu huo ndiye aliyewasilisha magari hayo kwa Waziri Matiang’i aliyeandamana na Waziri Msaidizi katika Wizara hiyo, Bw Patrick Ole Ntutu na Katibu wa Wizara Karanja Kibicho.

Shughuli hiyo iliendeshwa katika makazi rasmi ya Mshirikishi wa eneo la Kati. Magari hayo ni aina ya Toyota Land Cruiser TX na Mercedes Benz S350.

Bw Munga alisema hatua iliyochukuliwa na wakfu huo inalenga kurejeshwa sifa ya zamani ya utawala wa mkoa.

“Maafisa wa mkoa walikuwa watu wenye mamlaka makuu na ambao waliwakilisha Rais katika maeneo ya mashinani. Tunafaa kuwasaidia kwa kuwapa magari ya kuwawezesha kusafiri katika maeneo wanayosimamia kwa urahisi,” Bw Munga akasema.

Chini ya mpango huo, Washirikishi katika eneo zima la Mlima Kenya watapewa magari aina ya Mercedes Benz huku makamishna wa kaunti wakipewa magari aina ya Land Cruiser na Land Rover.

Magari hayo yataongezea yale ya serikali ambayo maafisa hao wamekuwa wakitumia.

Dkt Matiang’i alishabikia msaada huo huku akitoa wito kwa Wakenya wengine kuiga mfano huo kwa kuchangia katika uboreshaji wa utendakazi wa idara za serikali.

“Huu ni mfano mzuri na kielelezo cha uzalendo. Nyakati nyingi huwa tunalalamikia kutohusishwa kwa umma katika mipango ya serikali. Kila Mkenya ana uhuru wa kushiriki vitendo walivyofanya viongozi wa Wakfu huu,” akasema.

You can share this post!

ANGA YA KILIO: Mabaki ya ndege na miili ya watu 10...

Sonko amtimua waziri kwa kusafiri bila ruhusa yake

adminleo