• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 11:42 PM
Madhara ya kutumia dawa bila ushauri wa daktari

Madhara ya kutumia dawa bila ushauri wa daktari

Na MARGARET MAINA

[email protected]

MARA nyingi watu wanaugua maradhi mbalimbali, lakini wengi wao hawapendi kwenda hospitali kufanya vipimo au kupata ushauri wa kitaalamu kutoka kwa daktari.

Kutokana na uwepo wa dawa madukani, watu wengi wanapojisikia kuwa wagonjwa, hununua dawa kwenye maduka na kuanza kuzitumia.

Dawa zimetengenezwa mahususi ili kutibu maradhi fulani ambayo yatabainika kwa mgonjwa baada ya uchunguzi wa daktari.

Hivyo, matumizi ya dawa bila kufanya uchunguzi wa kitaalamu yanaweza kuwa na madhara makubwa kwenye afya yako.

Huongeza sumu mwilini

Dawa zimetengenezwa kwa kutumia kemikali mbalimbali ambazo kimsingi ni sumu inayoua vimelea vya magonjwa.

Sumu hii ya dawa ikizidi mwilini mwako inaweza kuleta athari mbalimbali kiafya.

Dawa hutengeneza usugu wa maradhi mwilini

Mtaalamu wa afya hutoa dozi ya dawa kulingana na vipimo na ugonjwa ulio nao.

Kutumia dawa bila bila ushauri kunaweza kusababisha vimelea vya ugonjwa vizoee dawa na kusababisha ugonjwa huo kuwa sugu. Maradhi kama vile malaria sugu na yale ya mfumu wa njia ya mkojo (UTI) sugu huja kwa sababu hiyo.

Dawa huweza kusababisha saratani

Dawa zinapoingia mwilini mwako bila utaratibu zinaweza kuharibu baadhi ya seli za mwili na kuzifanya kugeuka seli za saratani.

Dawa hupunguza kinga ya mwili

Kinga ya mwili ni ile hali ya mwili kuwa na uwezo wa kujikinga wenyewe dhidi ya maradhi mbalimbali.

Unywaji au utumiaji wa dawa unapunguza sana kinga ya mwili.

Ukiwa na kinga imara ya mwili, huwezi kuugua mara kwa mara.

Huweza kuathiri afya ya mama na mtoto

Mama mjamzito anatakiwa kuwa makini sana katika swala la kutumia dawa. Ni muhimu sana mama mjamzito anapohisi maradhi fulani kwenda kumuona mtaalamu wa afya kwa vipimo na kupatiwa tiba sahihi.

Dawa huweza kusababisha kifo

Dawa ni sumu zinazokabili vimelea vya magonjwa. Hivyo utumiaji wa dawa vibaya huweza kusababisha kifo. Hata kwa wagonjwa wa muda mrefu wanao tumia dawa, lazima wafuate ushauri wa daktari.

Hivyo ni muhimu kufanya uchunguzi pamoja na kutafuta ushauri wa kitabibu kabla ya kutumia dawa zozote kutibu maradhi yanayokukabili.

Ni muhimu na faida kubwa kuhakikisha kwamba unatumia virutubisho (Nutritional Supplements) kwa ajili ya kuboresha, kulinda na kuongeza kinga ya mwili.

You can share this post!

NIMETIMIZA NDOTO: Kipchoge anyakua dhahabu ya marathon

Mfanyakazi wa hoteli akana kuwahadaa wafanyabiashara...