• Nairobi
  • Last Updated April 24th, 2024 5:39 PM
Malaria kuua Wakenya elfu 44 juhudi zote zikielekezewa corona – WHO

Malaria kuua Wakenya elfu 44 juhudi zote zikielekezewa corona – WHO

Na PAULINE KAIRU

SHIRIKA la Afya Duniani (WHO), limeonya kuwa idadi ya vifo vinavyotokana na malaria huenda vikaongezeka maradufu Kenya na mataifa mengine ya Afrika kwani rasilimali nyingi zimeelekezwa kwa vita dhidi ya virusi vya corona.

Shirika la WHO linakadiria kuwa idadi ya vifo vinavyotokana na malaria itaongezeka hadi 769,000 barani Afrika mwaka 2020.

Jumla ya vifo 360,000 vya malaria viliripotiwa barani Afrika mnamo 2018, ambapo -Kenya ilipoteza watu 22,000 mwaka huo kutokana na malaria.

Kufikia sasa watu 14 wamekufa kutokana na Covid-19 nchini tangu mwezi Machi.

Mkurugenzi wa WHO barani Afrika Matshidiso Moeti, Jumamosi alihimiza mataifa ya Afrika kuendeleza juhudi za kukabiliana na malaria.

“Uchunguzi wa WHO umegundua kuwa ikiwa serikali za Afrika zitalegeza kamba katika vita dhidi ya malaria, vifo vinavyotokana na maradhi hayo vitaongezeka maradufu mwaka huu ikilinganishwa na 2018,” akasema afisa huyo.

Kiongozi wa kundi la waataalamu wa afya wanaoshughulikia malaria katika shirika la WHO, Dkt Akpaka Kalu, alisema kuwa dalili za ugonjwa wa corona na malaria zinafanana, hivyo huenda zikakanganya wahudumu wa afya.

Alitaka watu walio na dalili za virusi vya corona pia kupimwa malaria.

Alisema kuwa msimu huu wa mvua utasababisha ongezeko la visa vya malaria, na huenda waathiriwa wa ugonjwa huo unaoenezwa na mbu wakadhaniwa kuwa wagonjwa wa Covid-19.

“Tunahofia kuwa visa vya malaria vitaongezeka kwani mataifa mengi ya Afrika yanaingia kwenye msimu wa malaria. Visa vya malaria huwa vingi kati ya Julai na Septemba,”akasema.

“Ugonjwa wa malaria pia husababisha mwathiriwa kuwa na joto jingi sawa na virusi vya corona. Dalili nyingine za malaria ambazo hujitokeza kwa waathiriwa wa virusi vya corona ni uchovu, maumivu ya tumbo na kuhara. Hiyo ndiyo maana tunasema kuwa mtu akipatikana na joto jingi mwilini apimwe virusi vya corona na malaria,”akaongezea.

Shirika la WHO lilisema kuwa limepokea ripoti kuwa watu wanaoenda hospitalini wakiwa na malaria hawatibiwi na badala yake wanatumwa kupimwa virusi vya corona.

Idadi ya wastani

Mtu mmoja hufariki kutokana na maradhi ya malaria kila baada ya dakika mbili barani Afrika.

Wastani wa watu 200 milioni huugua malaria kila mwaka.

“Tumepokea ripoti kuhusu wahudumu wa afya wanaokimbia mgonjwa wa malaria anapofika hospitalini kutafuta matibabu ya malaria wakidhani ni corona,” akasema Dkt Kalu.

Kumekuwa pia na ripoti za wahudumu wa afya kuwapuuza watu wanaougua maradhi mengine wakisema wanashughulikia tu walio na corona.

You can share this post!

‘LOCKDOWN’: Rais apuuza Joho

Maaskofu wa kanisa Katoliki waitaka serikali itenge fedha...

adminleo