• Nairobi
  • Last Updated April 18th, 2024 8:55 AM
ManCity wamtia Harry Kane wa Tottenham mtegoni

ManCity wamtia Harry Kane wa Tottenham mtegoni

Na MASHIRIKA

TAFSIRI NA: CHRIS ADUNGO

MANCHESTER City wamewasilisha ofa rasmi ya Sh15.6 bilioni kwa ajili ya kushawishi Tottenham Hotspur kumwachilia fowadi Harry Kane kutua ugani Etihad.

Kane ni miongoni mwa washambuliaji wawili akiwemo Erling Braut Haaland wa Borussia Dortmund ambao wanaviziwa na kocha Pep Guardiola kwa malengo ya kujaza pengo la Sergio Aguero aliyeyoyomea Barcelona.

Hata hivyo, Dortmund wamesisitiza kwamba hawana nia ya kumtia Haaland mnadani ikizingatiwa kwamba wako radhi kuagana na Jason Sancho anayemezewa mate na Manchester United.Kane anahamu kuondoka Spurs, kikosi ambacho amekiwajibikia tangu akiwa mwanafunzi.

Kwa mujibu wa gazeti la Mirror Sport, Man-City ambao ni mabingwa wa Ligi Kuu ya Uingereza (EPL) watajiondoa katika vita vya kufukuzia maarifa ya Kane iwapo Spurs watakataa fedha ambazo wameziweka mezani kwa ajili ya maarifa ya Kane.

Kulingana na taarifa ya Man-City, kocha Guardiola hayuko radhi kusubiri hadi siku ya mwisho kumsajili Kane, 27. Matarajio yake ni kukamilisha mapema mchakato wa kusajili wachezaji wapya ili wawe sehemu ya maandalizi yao kabambe kwa ajili ya msimu mpya wa 2021-22.

Kinachosubiriwa sasa ni kuona iwapo Spurs ya mwenyekiti Daniel Levy itakubali ofa hiyo ya Man-City au la. Awali, Levy alisisitiza kwamba kikosi chochote kinachomezea mate huduma za Kane kingelazimika kuweka mezani kima cha Sh23 bilioni. Aidha, alishikilia kuwa Spurs wasingekuwa radhi kushuhudia Kane akijiunga na washindani wao wakuu kwenye EPL.

Tangazo la Kane kutaka Spurs wamwachilie mwishoni mwa Mei 2021 lilichochea vikosi vya Man-City, Man-United, Chelsea, Real Madrid na Barcelona kuanza kuyahemea maarifa ya mfumaji huyo raia wa Uingereza ambaye kwa sasa anawaniwa pia na Paris Saint-Germain (PSG) wanaotiwa makali na kocha Mauricio Pochettino aliyewahi kumnoa Kane kambini mwa Spurs.

Iwapo Man-City wataambulia pakavu kwenye vita vya kuwania Kane na Haaland, basi wamefichua mpango wa kumsajili nyota wa Southampton, Danny Ings.

 

  • Tags

You can share this post!

Peru wakung’uta Colombia huku Ecuador na Venezuela...

Denmark kumenyana na Wales kwenye muondoano wa Euro