• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 9:35 PM
Mariga ataka bangi ihalalishwe

Mariga ataka bangi ihalalishwe

LEONARD ONYANGO na ANITA CHEPKOECH

MGOMBEAJI ubunge katika uchaguzi mdogo wa Kibra kwa tiketi ya Chama cha Jubilee, Bw McDonald Mariga amesema atashinikiza uhalalishaji wa bangi kama atashinda kwenye kinyang’anyiro hicho cha Alhamisi.

Alisema hayo jana wakati kivumbi kilishuhudiwa kwenye kampeni za lala salama zilizoongozwa na Dkt William Ruto aliyeongoza kikosi cha Jubillee, na Bw Raila Odinga aliyeongoza kampeni za mgombeaji wa chama chake, Bw Benard Okoth.

Kikosi cha Jubilee kilikuwa katika Uwanja wa DC huku kile cha ODM kikikusanyika katika uwanja wa Joseph Kangethe, eneo la Woodley.

Pande zote mbili zilionyeshana ubabe kwa njia tofauti, ambapo mkutano wa Jubilee ulipambwa kwa burudani ya muziki kutoka kwa msanii wa regae kutoka Jamaica Kenyatta Hill akiwatumbuiza mamia ya watu waliofika uwanjani hapo.

Msanii huyo ndiye alimwongoza Bw Mariga kutoa wito wa kuhalalisha bangi.

“Tunajua shada (bangi) inatibu kansa kwa hivyo ni lazima tuisukume ihalalishwe. Hatutaki bangi ya kwenda kupiga watu ati umevuta shada. Shada ni dawa. Nataka mniingize bunge tuanze kutetea mambo ya shada,” akasema.

Wito wa kuhalalisha bangi kwa minajili ya matibabu ulikuwa ukivumishwa na aliyekuwa mbunge wa eneo hilo, marehemu Ken Okoth ambaye alifariki kwa kuugua saratani.

Katika mkutano wa ODM, Bw Odinga aliandamana na viongozi wengi wa vyama tofauti, wengi wakiwa ni wanaounga mkono handisheki kati yake na Rais Uhuru Kenyatta.

Miongoni mwao ni magavana Alfred Mutua (Machakos), Charity Ngilu (Kitui), Kivutha Kibwana (Makueni), James Ongwae (Kisii) na Anne Waiguru (Kirinyaga) pamoja na wabunge kadhaa akiwemo Maina Kamanda (Maalumu).

Katika eneo la Woodley, Bw Odinga alisema uchaguzi wa Kibra utakuwa mashindano kati ya handisheki na mrengo wa Tangatanga.

You can share this post!

Uhuru anahepa BBI?

Wanyimwa mlo kwa kusengenya bi harusi

adminleo