• Nairobi
  • Last Updated April 27th, 2024 6:55 AM
Mashindano ya Cecafa ya kina dada yaahirishwa hadi Agosti, Vihiga Queens kufunganya virago kurejea Vihiga

Mashindano ya Cecafa ya kina dada yaahirishwa hadi Agosti, Vihiga Queens kufunganya virago kurejea Vihiga

Na GEOFFREY ANENE

MAKALA ya kwanza ya mashindano ya soka ya klabu za kina dada ya Afrika Mashariki na Kati (Cecafa) ya kuingia Klabu Bingwa Afrika, yameahirishwa.

Mkurugenzi wa Baraza la Mashirikisho ya Soka ya Afrika Mashariki na Kati (CECAFA), Auka Gecheo amethibitishia gazeti la Taifa Leo mnamo Julai 14 kuwa tarehe mpya za mashindano hayo zitatangazwa hivi karibuni.

“Baada ya mashauriano, tumeamua kuwa mashindano ya kufuzu kushiriki Klabu Bingwa Afrika ya kinadada yaliyopangiwa kufanyika Julai 17 hadi Agosti 1 jijini Nairobi, hayaendelea jinsi yalivyopangwa,” alisema Mkenya huyo kabla ya kuongeza kuwa mashindano hayo sasa huenda yakapangwa kufanyika Agosti.

“Tutaketi chini na Shirikisho la Soka Afrika na Shirikisho la Soka Kenya (FKF) kuamua tarehe mpya. Kuna uwezekano mkubwa sasa yatafanyika Agosti,” Auka alisema Jumatano akithibitisha kuwa wenyeji Vihiga Queens watalazimika kurejea makwao hadi tarehe mpya zitakapotangazwa.

Cecafa ilifaa droo ya mashindano hayo juma lililopita, ingawa Shirikisho la Soka nchini Rwanda (FERWAFA) liliamua kuondoa wawakilishi wake Scandinavia likisema limechukua hatua hiyo kwa sababu ya changamoto za ugonjwa wa Covid-19 nchini humo.

Mabingwa hao wa Rwanda walikuwa wametiwa katika Kundi C pamoja na FAD (Djibouti) na wenyeji Vihiga Queens.

Timu nyingine zilizopangwa kuwania tiketi moja ya kuingia Klabu Bingwa Afrika ni Lady Doves (Uganda), PVP (Burundi), Simba Queens (Tanzania), Commercial Bank of Ethiopia (Ethiopia), Yei Joint Stars (Sudan Kusini) na New Generations (Zanzibar). Vihiga Queens iliyowasili jijini Nairobi mnamo Julai 7 kwa mashindano hayo, sasa itarejea nyumbani katika kaunti ya Vihiga.

You can share this post!

Manchester United kukosa huduma za fowadi Rashford kwa...

Jinsi tunavyoweza kuimarisha umiliki wa vipande vya ardhi,...