• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 11:42 PM
MILA NA DESTURI: Utoaji mahari na ndoa katika jamii ya Wasomali

MILA NA DESTURI: Utoaji mahari na ndoa katika jamii ya Wasomali

Na FARHIYA HUSSEIN

[email protected]

ILIKUWA fahari kubwa Taifa Leo kupata kupata fursa ya kujumuika na jamii ya Wasomali eneo la Kaskazini Mashariki, Kaunti ya Garissa kushuhudia jinsi harusi zao za kitamaduni zinavyofanywa.

Makaribisho ni mazuri katika uwanja mmojawapo. Shangwe na vigelegele vinahanikiza huku sauti nyororo za kina mama wakiimba nyimbo za kitamaduni zikizidi kunogesha uhondo.

Tunapatana na Bw Deqow Ali na mke wake Bi Barwaqa Adow ambaye anamtayarisha binti yao atakayefunga ndoa siku chache zijazo.

Binti yao karibu ataolewa katika harusi ya kitamaduni.

Bi Adow anasema harusi ni mojawapo ya tamaduni muhimu zaidi kwa jamii ya Wasomali.

“Harusi kwetu huashiria umoja pale nyoyo za wawili wapendanao zinakuja pamoja kutengeneza uhusiano baina ya familia hizo mbili,” anasema Bi Adow.

Bi Barwaqa Adow akitayarisha chakula nje ya nyumba yake ya kitamaduni. Picha/ Farhiya Hussein

Wasomali wanafahamika kwamba wao ni wa Kishiti (cushites) na wanapatikana zaidi Kaskazini Mashariki mwa Kenya.

Asili yao inaelezwa kwamba ni wa kutoka mkoa wa Ogaden, Kusini mwa Ethiopia.

Wasomali zaidi ya 500,000 wanaishi Kaskazini Mashariki, Kenya.

Familia nyingi za Kisomali zinazopatikana nchini Kenya ni zile za Ajuran na Ogaden na lugha yao ni ya Kisomali.

Ingawa hivyo, kunao wengine ambao pia wanazungumza lugha ya Kisomali na wanaitwa Garreh lakini si Wasomali kamili kwa sababu wamechanganya damu ya Borana.

Wasomali hujulikana kuwa ni wafugaji hasa wa ngamia, mbuzi, kondoo, na ng’ombe.

Wakigawanywa katika makundi tofauti ya kikoo – clans – wanapatikana Hawiye, Degoodiya, Ajuuraan, Isxaaq na Ogaadeen .

Wengi wao hupatikana sana jijini Nairobi, Mombasa na sehemu za Kaskazini Mashariki mwa Kenya.

Bw Ali anaelezea kuwa kuna methali katika lugha ya Kisomali inayosema “bahati ni wakati fursa inakutana na maandalizi” na ndivyo huwa wanaashiria wanaoelekea kufunga ndoa.

Bibi arusi kutoka jamii ya Wasomali akivishwa kitambaa na wanawake wa jamii kama njia ya kumpokeza baraka kwenye maisha yake ya ndoa. Picha/ Farhiya Hussein

Anafafanua kwamba katika jamii ya Wasomali, utoaji wa mahari – Meher – hufanyika siku chache kabla ya harusi na wakati mwingine hufanyika siku hiyo ya ndoa.

Ukweli ni kwamba ni jambo linalohitaji mtu kujikusuru na kujitolea kikamilifu. Si rahisi kwa upande wa bwana harusi kwani anapaswa kushughulikia familia ya bi harusi na na kuitunuka zawadi.

Bw Ali (babake biarusi) na ndugu zake walipokea kutoka kwa familia ya bwana harusi zawadi ikiwa ni pamoja na mtoto wa ngamia, hela zilizofunikwa kwa kitambaa ghali na ngamia 20 kama malipo ya mahari.

“Kuna zawadi nne kubwa ambazo bwana harusi anapaswa kutoa. Ya kwanza tunaita, Gabaati ambayo inahusisha nirigi – mtoto wa ngamia – na kawaida huletwa na bwana harusi na baba yake wanapokuja kuomba bi harusi. Ya pili ni Yarad ambayo ni zawadi inatolewa siku ya utoaji mahari ya kuthamini biarusi (Kawaida ni pamoja na pesa zilizofunikwa kwa kitambaa ghali). Tatu, Sooryo; pesa wanazopewa wanaume wa familia ya biarusi ama ndugu au binamu. Na mwishowe, bwana arusi huleta ngamia kama shukrani kwa kuruhusiwa kumuoa yule biarusi,” akaelezea Bw Ali.

Lakini alieleza kadri siku zinavyosonga utamaduni unapotea polepole.

Zama zile, biarusi angetolewa ngamia 100 kama mahari lakini sasa bwana harusi anaruhusiwa kulipa ngamia 10 kama mahari.

Wasomali wana historia pevu ya ufugaji wa ngamia. Picha/ Farhiya Hussein

“Bila malipo ya mahari hakuna arusi ambayo itafanyika na ina maana kwamba biarusi anapaswa kuwa wazi juu ya kile anataka na bila shaka bwana arusi atawajibika na kukitoa,” akasema Omar Abdullahi, mmoja wa wazee wa baraza katika kijiji hicho.

Harusi za Wasomali, nyingi hufanywa kabla ya jua kutua na hufanyika maeneo ambayo kila mtu ambaye huwa amealikwa kwa tarehe iliyowekwa anaweza kufika.

Taifa Leo ilipata fursa ya kushuhudia ndoa ya bintiye Bw Ali.

Wanawake walijitokeza wakiwa wamevalia mavazi yao ya rangi ijulikanayo kama baati. Ni kubwa, na hung’aa (glitters) na hutengenezwa kwa hariri. Nguo hizo ni kubwa kiasi kwamba wanawake hushikilia upande mmoja wakati wa kucheza na kuimba.

Wanawake basi wanamsindikiza biarusi kuelekea kwenye chumba ambacho kimejengwa maalum kwa wanandoa hao wapya huku wakipiga makofi na kucheza wakati wanapiga ngoma.

Bwana arusi anaonekana amesimama kwa umbali nje ya chumba hicho.

Kisha kundi la wanaume linakuja polepole huku wakiimba nyimbo za sifa na kucheza wakielekea kwenye hicho chumba, ambapo bibi arusi yuko.

Ndani ya kile chumba kumetandikwa shuka ndefu chini. Bi arusi amekalishwa katikati huku wanawake wakimzunguka na kuimba.

Wanawake wengine hukusanyika nje ya chumba, wakiacha nafasi ya kutosha kwa wanaume wanaokaribia.

Wanaume kisha hufika pale, wakiongozwa na wazee wa kijiji wanamzunguka bwana arusi kama kundi la nyuki.

Ndani ya chumba hicho, wanandoa hao wapya wanapitia mila kadhaa ikiwa ni pamoja na Todoba Bax, Xeedho, Shaash saar.

Kutumia kitambaa kipepesi wanawake huweka kitambaa juu ya kichwa cha biarusi ambacho huashiria baraka na kumtakia heri katika ndoa yake.

“Hii inategemea na ukoo na mbari ambapo bwana arusi na biarusi hutoka. Wengine huoana kutoka katika familia moja. Kulingana na ukoo, wale wanaofunga ndoa wanaweza kuhusishwa kupitia wazazi wao. Kwa mfano, mama ya bwana arusi na baba ya biarusi wanaweza kuwa wa kutoka kwa tumbo moja,” akabainisha Bw Ali.

Katika jamii zingine nchini, hii inaweza kuonekana kama mwiko yaani taboo.

Utamaduni wa Kisomali pia unaruhusu mwanamume kuoa hadi wake wanne; hasa chini ya sheria za Kiislamu.

You can share this post!

Sanchez ana risasi moja pekee ya kujiokoa Inter Milan

Corona yachangia uhaba wa damu katika hifadhi Mombasa

adminleo