• Nairobi
  • Last Updated April 25th, 2024 10:06 AM
Mwangi Wa Iria aahidi kuachia Murang’a uchumi wa maparachichi wa hadi Sh32bn

Mwangi Wa Iria aahidi kuachia Murang’a uchumi wa maparachichi wa hadi Sh32bn

Na MWANGI MUIRURI

GAVANA wa Murang’a, Mwangi wa Iria ameahidi kugeuza Kaunti hiyo kuwa ya uchumi wa maparachichi aina ya Hass ambapo analenga kuzidisha idadi ya miche ya zao hilo hadi 10 milioni akivuka mwaka wa 2023.

Ameambia Taifa Leo katika mahojiano kuwa kwa sasa idadi ya miche ya maparachichi eneo hilo imesimamia kwa 6 milioni na atakuwa akiwapa wakulima wake miche 1 milioni kila mwaka hadi mwaka 2022.

Alisema kuwa kwa sasa pato la ujumla kutokana na zao hilo ni Sh2.5 bilioni kwa mwaka, akiahidi kuwa pato hilo linafaa kupaa mwaka wa 2025 ambapo ile miche atakuwa amepeana hadi mwaka wa 2022 itakuwa imeungana pamoja kwa mavuno.

“Kwa kuwa miche ya Hass huchukua miaka mitatu ndipo ianze kuzaa mavuno ya uhakika.Ile tutakuwa tumepeana mwaka wa 2022 itakuwa imeanza kuvunwa mwaka wa 2025 na ndipo mavuno yote ya miche 10 milioni yatajumuishwa pamoja kama utajiri wa kaunti sokoni,” akasema Wa Iria.

Alisema kuwa mti mmoja wa Hass ukikomaa unaweza ukatoa maparachichi 1, 000 kumaanisha kuwa miche 10 milioni inaweza ikatoa maparachichi 1 bilioni.

“Sokoni, bei ya tunda moja la Hass kulingana na gredi huwa katika kiwango cha kati ya Sh8 na Sh32. Hii ina maana kuwa tunaweza tukaafikia pato la ujumla la kati ya Sh8 bilioni na Sh32 bilioni,” akasema.

Ushirika

Alisema kuwa kwa sasa ameunganisha wakulima 250, 000 katika vikundi vya uzalishaji Hass na ambapo wako katika makundi ndani ya wadi zao na hatimaye kuunda muungano mmoja wa ushirika wa Kaunti.

Alisema kuwa muungano huu umesaidia sana katika kuwafikia wakulima na vifaa muhimu na pia kusaka soko la uhakika na pia kupiga vita upenyo wa madalali katika sekta hii ya maparachichi.

Alisema kuwa kwa sasa bei imeimarika katika soko la Ulaya na pia la Bara Asia akiongeza kuwa kwa sasa serikali yake itaweka mikakati ya kuwasaidia wakulima hao kuafikia masharti ya soko la kimataifa.

You can share this post!

Wacheza kamari, walevi wafinywa

Tupo tayari kwa kipute na DRC, Stars wajitanua

adminleo