NA LEONARD ONYANGO
KINARA wa Azimio Raila Odinga anakabiliwa na mzigo mzito huku akiendeleza juhudi zake za kupambana na serikali.
Bw Odinga ana kibarua kigumu cha kuhakikisha kuwa Rais Mstaafu Uhuru Kenyatta pamoja na wandani wake hawaangaishwi na serikali ya Kenya Kwanza.
Bw Odinga amekuwa katika mstari wa mbele kushutumu serikali kwa kujaribu kuhangaisha familia ya Rais Mstaafu Kenyatta kwa kisingizio cha kutolipa ushuru.
Jumatano, Bw Odinga alikuwa wa kwanza kufika nyumbani kwa aliyekuwa waziri wa usalama Fred Matiang’i aliyedai kuvamiwa na maafisa wa polisi.
Duru katika Idara ya Kuchunguza Uhalifu (DCI) zilidokezea Taifa Leo kuwa mawaziri watatu wa serikali ya Bw Kenyatta wanachunguzwa kwa madai ya ufisadi na kukwepa ushuru.
Miongozi mwa mawaziri wanaochunguzwa ni Dkt Matiang’i.
Alhamisi, Mkurugenzi wa DCI Mohamed Amin alisema kuwa japo Dkt Matiang’i anachunguzwa hawajafikia hatua ya kumkamata.
Bw Odinga pia anaandamwa na kibarua kigumu cha kuzuia uasi ndani ya Azimio na chama chake cha ODM.
Viongozi wa ODM, wakiwemo wandani wake wa karibu kama vile Mbunge Maalumu John Mbadi, wamekuwa wakionyesha uasi wazi.
Bw Odinga pia yuko hatari ya kusalia pweke kufuatia mapinduzi ndani ya chama cha Jubilee ambapo Katibu Mkuu wa chama hicho ‘alipinduliwa’ jana Ijumaa.
Waziri Mkuu huyo wa zamani pia anakabiliwa na kazi ngumu ya kupambana na serikali ya Kenya Kwanza ndani na nje ya Bunge huku idadi kubwa ya wabunge wake wakionekana kuunga mkono Rais Ruto.
Jana Ijumaa, Bw Odinga aliyekuwa akizungumza katika eneo la Mavoko, Kaunti ya Machakos, alishikilia kuwa hatambui serikali ya Kenya Kwanza na Rais Ruto akisisitiza kuwa alishinda uchaguzi wa Agosti 9, 2022.
Wakenya pia wameweka matumaini makubwa kwa Bw Odinga kuwatetea kufuatia kuongezeka kwa bei ya chakula na bidhaa nyinginezo muhimu.
Aidha Bw Odinga aliwataka Wakenya wanaoumizwa na gharama ya juu ya bidhaa kujitokeza na kuandamana kushinikiza serikali kuchukua hatua.
“Watu wana njaa na wanahitaji chakula, maji na dawa,” akasema Bw Odinga.
Kiongozi wa ODM pia anakumbwa na presha ya kumtaka kustaafu kutoka kwenye siasa.
Bw Odinga, hata hivyo, ameshikilia kuwa angali na nguvu na hana mpango wa kustaafu hivi karibuni.
Subscribe our newsletter to stay updated