• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 7:00 PM
NASAHA ZA RAMADHAN: Aliyefunga azingatie zaidi Ucha Mungu katika mwezi wa Ramadhani

NASAHA ZA RAMADHAN: Aliyefunga azingatie zaidi Ucha Mungu katika mwezi wa Ramadhani

Na ATHMAN FARSI

MPENDWA msomaji wa ukumbi huu wa Nasaha za Ramadhani, leo naomba tuangazie amali (matendo) bora katika mwezi huu wa Ramadhani.

Mijadala itakuwepo kuwa ni ibada hii ama ile ambayo ni muhimu ama bora zaidi lakini kwa mujibu wa Bwana Mtume Muhammad (s.a.w) alipokhitimisha khotuba yake ya Ijumaa ya mwisho ya mwezi wa Shaaban, Ali bin Abitalib (a.s) anatuambia; “Baada ya kumaliza Mtume (s.a.w) hotuba hiyo, “nikasimama na nikamuuliza, ‘Ya Rasuu-lallaah, Amali gani bora kabisa katika mwezi huu mtukufu?’ Akajibu, ‘Uchaji wa Mwenyezi Mungu kwa kila kilichoharamishwa na kukatazwa’”.

Uchaji Mungu ni neno dogo sana na fupi mno lakini maana na upeo wake ni mkubwa zaidi na ni ngumu kivitendo. Kuswali suna, kusoma Qur’ani, kulisha masikini, miongoni mwa mambo mengine ya kheri hayawezi kuwa sawa kabisa na Uchaji Mungu. Yote hayo ni sehemu moja tu ya uchaji Mungu. Kujitenga na madhambi na alichoharamisha Mwenyezi Mungu ni jambo la wajibu, si mwezi wa Ramadhani tu bali ni katika maisha yote ya mtu.

Kumcha Mungu huandamana na subira na uvumilivu. Kwa mfano mtu akiwa amefunga na majira ya saa kama kumi na moja jioni. Mtu akaja kumkejeli na kumtusi tusi kubwa, ikiwa hana subira basi itabidi audhike na kumjibu kwa matusi na hata kumchapa mwenye kumtusi. Ikiwa unamcha Mungu kisawa sawa, atamkumbuka Mola wake mara moja na atampuuza huyo.

Anayemcha Mungu anaamini mambo ya Mwenyezi Mungu yasiyoonekana kwa macho, hutekeleza swala kwa wakati wake, hutoa kwa ajili ya Mola wake, anaamini aliyoteremsha Allah (s.w.t), huwa na yakini na siku ya mwisho. Muumini pia hustahamili na kusibiri nyakati za raha na shida, ni mwenye kutimiza ahadi, na mwenye kuomba msamaha kwa Mola wake kila wakati,

Kwa hivyo, mwenye kuacha kila alichoharamisha na kufuata aliyoamrisha kwa yakini, mtu huyu atakuwa amefanya amali bora kuliko yote na huku ndiko kumcha Mungu.

You can share this post!

Joho akariri Umoja wa Pwani ungalipo

Rais wa Chad afariki vitani baada ya kuchaguliwa tena