NA MWANGI MUIRURI
MBUNGE wa Maragua Bi Mary wa Maua amedai kwamba baadhi ya hospitali katika Kaunti ya Murang’a wagonjwa wamo katika hatari ya kuliwa na panya kwa sababu ya uchafu.
“Hospitali kuu ya Maragua kwa mfano iko katika hali mbaya sana…Wagonjwa wanaweza wakaumwa na panya. Tunataka hali hiyo ilainishwe na viwango vya afya viimarishwe,” akasema.
Bi wa Maua aliteta kwamba sekta ya afya ni mojawapo ya zile muhimu sana katika huduma kwa wananchi, hivyo basi waliopewa majukumu wanapaswa kuwajibikia rasilimali kwa umakinifu.
Tayari, Seneta wa Murang’a Bw Joe Nyutu ameitaka kamati maalum kuhusu afya katika bunge la Seneti kuchunguza hali ya miundo mbinu na huduma za Afya katika Kaunti ya Murang’a.
Kamati hiyo ambayo huongozwa na Seneta wa Uasin Gishu Bw Jackson Mandago tayari imezuru baadhi ya hospitali za Murang’a kujifahamisha na hali ilivyo.
“Hatutakubali Kaunti yetu iwe ndiyo ngome ya wagonjwa kuaga dunia kwa kukosa huduma muhimu kama hewa ya Oxijeni ndani ya wadi na pia ukosefu wa huduma za ambulensi,” akasema Bw Nyutu.