• Nairobi
  • Last Updated April 19th, 2024 8:55 PM
Roberto Martinez pua na mdomo kuteuliwa kocha wa timu ya taifa ya Ureno

Roberto Martinez pua na mdomo kuteuliwa kocha wa timu ya taifa ya Ureno

Na MASHIRIKA

KOCHA Roberto Martinez yuko pua na mdomo kupokezwa mikoba ya timu ya taifa ya Ureno.

Mhispania huyo amekuwa akishiriki mazungumzo na Shirikisho la Soka la Ureno kwa nia ya kujaza pengo la mkufunzi Fernando Santos aliyejiuzulu baada ya Ureno kubanduliwa na Morocco kwenye robo-fainali za Kombe la Dunia 2022 nchini Qatar.

Martinez pia alibwaga manyanga kambini mwa Ubelgiji baada ya miamba hao kudenguliwa mapema kwenye Kombe la Dunia katika hatua ya makundi nchini Qatar.

Martinez ambaye ni kocha wa zamani wa Everton na Wigan Athletic aliteuliwa kuwa kocha wa Ubelgiji mnamo 2016 na mkataba wake ulitarajiwa kutamatika mwishoni mwa fainali za Kombe la Dunia za 2022 nchini Qatar.

Ubelgiji walioambulia nafasi ya tatu nyuma ya Croatia na Ufaransa kwenye fainali za Kombe la Dunia za 2018 nchini Urusi walianza kampeni za kipute hicho mnamo 2022 wakishikilia nafasi ya pili duniani kwa mujibu wa viwango bora vya Shirikisho la Soka Duniani (FIFA).

TAFSIRI NA: CHRIS ADUNGO

  • Tags

You can share this post!

Shirikiana ndio, lakini msimezwe na Ruto, Raila aambia...

DARUBINI YA WIKI: Toleo Nambari 19 | Januari 8, 2023

T L