• Nairobi
  • Last Updated April 18th, 2024 2:37 PM
Shaffie Weru sasa afukuza Sh21 milioni akidai alipigwa kalamu kupitia WhatsApp

Shaffie Weru sasa afukuza Sh21 milioni akidai alipigwa kalamu kupitia WhatsApp

NA MWANGI MUIRURI

Aliyekuwa Mtangazaji wa kituo vcha Radio cha Homeboyz Shaffie Weru, amezindua harakati za kuvuna Sh21 Milioni kutoka kwa aliyekuwa mwajiri wake wa hadi wiki jana—Radio Africa Group—akisema kuwa alifutwa kazi kwa njia haramu.

Kupitia kwa kampuni ya mawakili ya MMA, Shaffie ameandaa hisibati kwamba kutokana na mshahara wake wa kila mwezi uliokuwa Sh682,500 uhesabiwe kwa miezi 12 ndio ridhaa ijumuike kwa kiwango cha Sh8.1 Milioni na kisha na kisha ahesabiwe kiinua mgongo cha kiwango sawa na mshara huo wake wa kila mwezi kwa kila mwaka ambao amehudumia mwajiri huyo na hatimaye aishie kuvuna Sh21.1 Milioni.

Shaffie anashikilia kuwa alifutwa kazi mwendo wa saa 11 usiku kupitia ujumbe wa WhatsApp huku kanuni za Wizara ya Leba zikihitaji apokezwe ujumbe kwa njia rasmi, na hii iwe ni baada ya kupewa ilani inayoishia kupewa nafasi ya kujitetea baada ya kufahamishwa kuhusu kiini cha tetesi za kuhitaji kuadhibiwa, na hayo yote yafanyike katika siku na masaa ya kazi.

Shaffie alijipata taabani wiki jana akiwa na watangazaji wake wawili katika shoo yao ya asubuhi ikifahamika kama ‘The Lift-Off’ ambapo walizindua mjadala ulioashiria kuwalaumu wahanga wa ukatili dhidi ya wanawake.

Akiwa pamoja na Neville Musya na DJ Joseph Munoru anayefahamika kama Joe Mfalme walikashifiwa pakubwa kwa shoo hiyo yao ambapo mada ilikuwa kuhusu mwanamke aliyetambulika kama Eunice Wangare aliyesukumwa kutoka gorofa la 12 na mwanamume kwa jina Moses Gatama Njoroge.

Wawili hao waliripotiwa kuwa walikutana kwa mara ya kwanza kwa nia ya kujenga uhusiano wao uliokuwa umezinduka kutoka mtandao wa Facebook lakini mwanamume akageuka kuwa fisi aliyetaka kuonja asali Pap. Mrembo akikataa na ndipo kwa hasira, akasukumwa nje ya gorofa hilo na akaishia kuwa na majeraha mabaya mwilini—mjadala ukiwa uwezekano wa kuanguka kutoka urefu huo na bado ubakie hai kusimulia yaliyojiri.

Shaffie anadaiwa kuwa alinukuliwa kuwaongoza wenzake Studioni kuwataka Wanawake wawe na ujanja wa kutokubali kunaswa haraka hadi usiri wa nyumba ya mwanamume kwa kuwa hilo huwaangazia kama wasio na maadili kuhusu husiano za kimapenzi au waliopoteza imani ya kuwahi kupendwa.

Alisema kuwa kujianika kwa msingi huo wa kuwa na haraka ya kupendwa na kuwa karibu na kitanda cha anayemchumbia ndio kiini cha kukumbwa na ukatili sawa na huo uliokabidhiwa Bi Wangare.

Katika taarifa ya Machi 27, kampuni hiyo ya Radio Africa Group ilisema kuwa tayari ilikuwa imewafuta kazi watatu hao huku naye Shaffie akiomba msamaha katika mtandao wake wa Twitter ambapo alikiri kunoa katika tafsiri yake ya hali hiyo ya dhuluma dhidi ya Bi Wangare na wanawake wote kwa ujumla.

Shoo hiyo ilikuwa imezua hasira kuu mitandaoni ya kijamii huku kilio cha umma kikifikia serikali na ambayo iligonga kituo hicho kwa kukitoza faini ya Shilingi Moja Milioni na hatimaye kupiga marufuku shoo hiyo kwa kipindi cha miezi sita, huku nayo Kampuni ya East African Breweries ikitangaza kuondoa uthamini wa kimatangazo katika shoo hiyo ikiteta.

Kwa sasa, Shaffie analenga kuvuna katika sarakasi hiyo na ambapo akifanikiwa, atakuwa kama aliyebahatika katika mchezo wa kamari.

You can share this post!

SULUHU APATA MPANGO TZ

Ninafurahia BBI imesambaratika, tuliomba Mungu sana –...