• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 8:50 AM
Shanzu United FC yadondosha alama tatu dhidi ya wenyeji Ziwani Youth

Shanzu United FC yadondosha alama tatu dhidi ya wenyeji Ziwani Youth

Na CHARLES ONGADI

MASAIBU ya Shanzu United FC katika Ligi ya Taifa Daraja la Pili yaliendelea mwishoni mwa juma walipokung’utwa 1-0 na Ziwani Youth uwanjani Tudor Primary, Mombasa, Jumamosi.

Shanzu United inayofunzwa na Mody Musa, mchezaji wa zamani wa Mafuko Bombers FC, ilipigiwa upatu kuibuka na ushindi mkubwa katika pambano hilo.

Hata hivyo, kinyume na matarajio ya wengi, wenyeji Ziwani Youth walitumia vyema uwanja wao wa nyumbani kwa kutangulia kupata bao la mapema kupitia Yusuf Kamanza katika dakika ya nane.

Mastraika wa Shanzu United wakiongozwa na mfungaji wa mabao mengi katika ligi hii Heri Juma, walijaribu katika kipindi cha kwanza kusawazisha bao hilo bila kufaulu.

Licha ya kupata nafasi nyingi , wachezaji wa Shanzu United walishindwa kubadilisha nafasi hizo kuwa mabao.

Katika dakika ya 67 , mshambulizi matata Heri Juma alipachika bao la kusawazisha ila tu kwa refa wa pambano hili Francis Mariga kulikataa kwa madai kwamba aliotea .

Wachezaji wa Ziwani Youth waliamua kulinda bao hili katika kipindi chote cha pili na kuzima kabisa juhudi za washambulizi wa Shanzu United kupata bao.

Wachezaji wa Ziwani Youth na Shanzu United waking’ang’ania mpira katika pambano la Ligi ya Taifa Daraja la Pili uwanjani Tudor Primary, Juni 26, 2021. Picha/ Charles Ongadi

Katiia mechi yao wikendi iliyopita, Ziwani Youth iliandikisha matokeo ya sre ya 2-2 na Progressive FC ya Malindi katika mechi iliyochezwa katika uwanja huo huo wa Tudor Primary.

Akizungumza na Taifa Leo baada ya pambano, kocha mshikilizi wa Ziwani Youth Mselem Abdallah aliwapongeza mno wachezaji wake.

“Tumecheza bila wachezaji wetu muhumu walio katika listi ya majeruhi na tumepata ushindi huu ijapo ni mwembamba,” akasema Abdallah.

Lakini kulingana na meneja wa Shanzu United James Sewe, wachezaji wake walicheza vyema lakini wakakosa bahati.

Shanzu United imeratibiwa kupepetana na Tikki FC uwanjani Shanzu Teachers Collage wakati Ziwani Youth ikisafiri hadi Kilifi kuchubuana na Bahari FC uwanjani Mtwapa Primary.

You can share this post!

Cecafa U23 yaahirishwa kutoka Julai 3 hadi Julai 17

Dalili za upungufu wa maji katika ngozi