• Nairobi
  • Last Updated April 19th, 2024 1:14 PM
WASONGA: Sherehe bila kusaidia familia za mashujaa ni kazi bure

WASONGA: Sherehe bila kusaidia familia za mashujaa ni kazi bure

Na CHARLES WASONGA

HUKU Kenya ikisherehekea Siku Kuu ya Mashujaa leo Jumatano, ni aibu kwamba jamaa za wapiganiaji ukombozi, wa kwanza, wa taifa hili wanaishi katika hali ya uchochole.

Ama kwa hakika watu hawa hawaoni thamani ya sherehe za leo kwa sababu hawafurahii matunda ya machozi, jasho na damu waliomwaga mababu zao waliopigania uhuru wa Kenya.

Isitoshe, serikali ya sasa imewatelekeza mashujaa wachache wa ukombozi ambao wangali hai, kutokana na kudura za mwenyezi Mungu.

Kile ambacho serikali hufanya kila mwaka ni kutaja majina yao katika sherehe za kitaifa kisha kuwaalika kwa dhifa ya chakula cha jioni katika Ikulu ya Nairobi.

Japo kuna sheria inayotoa mwongozo wa namna serikali inapaswa kushughulikia masilahi ya aina mbalimbali ya mashujaa, serikali haijafanya lolote.

Kwa mfano, kuna Baraza la Kitaifa la Mashujaa ambalo lilipaswa kutekeleza mapendekezo ya sheria.

Baraza hilo lenye wanachama 13 lilitarajiwa kutengewa Sh300 milioni za kusaidia mashujaa na familia zao lakini pesa hizo hazijatolewa tangu sheria hiyo ilipopitishwa mnamo 2014.

Juzi, kiongozi wa ODM Raila Odinga alimtembelea mjane wa shujaa wa ukombozi wa Kenya, Dedan Kimathi, Mama Mukami Kimathi akiahidi kumsaidia anunue kipande cha ardhi katika Kaunti ya Laikipia.

Bw Odinga aliungama kuwa serikali ilikuwa imeahidi kutoa Sh60 milioni kwa ajili ya ununuzi wa ardhi hiyo, lakini pesa hizo hazijatolewa hadi wakati huu.

Ama kwa hakika ni aibu kubwa kwamba mkewe Kimathi anaishi katika nyumba ya kukodisha katika mtaa wa Komarocks, Nairobi kwa kukosa ardhi ya kujengewa makazi ya heshima.

Kinaya ni kwamba, mumewe alipigania jino kwa ukucha hadi wazungu wakakubali kuachilia ardhi ya Waafrika walionyakua.

Mnamo Agosti 31, 2021 Rais Uhuru Kenyatta aliomboleza kifo cha bintiye Mama Kimathi, bila kutaja mipango yoyote ambayo serikali imeweka kuisaidia familia hiyo.

Mnara wa Dedan Kimathi ulioko katika barabara ya Kimathi, Nairobi hauna maana yoyote ikiwa familia ya shujaa itaendelea kuishi katika ufukara.

Isitoshe, ujenzi wa Mnara wa Mashujaa unaendelea katika bustani ya Uhuru Gardens, Nairobi hauna maana yoyote ikiwa familia za mashujaa mbalimbali nchini zitaendelea kutelekezwa na serikali iliyoko mamlakani sasa.

Sherehe za leo Jumatano katika Uwanja wa Michezo wa Wanguru, Kaunti ya Kirinyaga hazitakuwa na maana yoyote ikiwa mashujaa hawa watamiminiwa sifa bila serikali kutangaza mipango madhubiti ya kuwasaidia pamoja na familia zao.

You can share this post!

NGILA: Tumia ufadhili wa Google kupiga jeki biashara yako

Korti yaelezwa jinsi mwanamke alivyoibia mfanyabiashara

T L