NA HELLEN SHIKANDA
RAIS William Ruto ameendelea kuelezea matumaini yake kwamba mataifa kote duniani yatazinduka na kuanza kutekeleza kwa vitendo hatua zinazolenga kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi.
Akihutubu Jumanne kwenye Ukumbi wa Jumba la Mikutano ya Kimataifa la Kenyatta (KICC) jijini Nairobi katika Siku ya Pili ya Kongamano Kuu la Afrika la Kuangazia Mabadiliko ya Tabianchi (ACS23), Rais Ruto amesema vijana wakipewa nafasi wana fursa ya kusaidia pakubwa katika juhudi za kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi.
“Ni fahari kuu kwamba mimi ni mwenyekiti wa kamati ya viongozi wa Afrika inayoangazia mabadiliko ya tabianchi. Mnamo Jumapili vijana waliandaa kongamano na tuliona namna walivyo na uwezo wa kubadili dunia kuwa pahala salama wakipewa nafasi,” amesema Rais Ruto.