• Nairobi
  • Last Updated April 18th, 2024 6:27 PM
Takwimu: Siaya yaongoza kwa idadi kubwa zaidi ya vifo nchini

Takwimu: Siaya yaongoza kwa idadi kubwa zaidi ya vifo nchini

Na DOROTHY OTIENO na JOSHUA MUTISYA

IKIWA unaishi Siaya, una uwezo mkubwa zaidi kufariki kabla ya muda wako ikilinganishwa na yeyote anayeishi katika kaunti nyingine nchini Kenya, utafiti wa Nation Newsplex umebaini.

Kulingana na utafiti huo, idadi ya vifo ni asilimia 20 miongoni mwa wananchi 1,000 mwaka wa 2016, huku mkazi wa Siaya akiwa na uwezo mara tatu wa kuaga dunia akilinganishwa na mkazi wa Nairobi.

Jiji la Nairobi lina idadi ndogo zaidi ya watu wanaoaga dunia, ambapo ni watu sita kati ya 1,000. Hali hiyo imeshuhudiwa Siaya tangu 2011 ambapo kila mwaka huongoza kwa idadi ya vifo.

Kwa kipindi hicho, Nairobi imeorodheshwa miongoni mwa kaunti tatu ambazo zina idadi ndogo zaidi ya vifo nchini katika kipindi hicho.

Kwa kuzingatia visa vya watu wanaoua wengine, Kaunti ya Siaya iliorodheshwa ya saba. Kitaifa, visa hivyo ni 14 kati ya 100,000.

Kaunti zingine tatu Nyanza zimo miongoni mwa kaunti 10 za mbele zilizo na idadi kubwa ya vifo kwa watu 1,000.

Kisumu imeorodheshwa ya tano ambapo ina viwango vya vifo kuwa asilimia 14.1, Homabay ni ya saba kwa asilimia 13.5 na kufuatwa na Migori kwa asilimia 13.
Kaunti ya pili ni Vihiga ambayo idadi ya vifo ni 17 kwa watu 1,000 na kufuatwa na Elgeyo-Marakwet(15) na Taita Tavet(14.7).

Vihiga imekuwa nambari hiyo tangu 2011. Kaunti ya Turkana imo katika nafasi ya sita(14) na Bungoma imo nambari tisa(12.4).

Kaunti ya Kakamega ni nambari 10 (12). Idadi ya mauaji kwa watu 100,000 katika Kaunti ya Vihiga ni 11, ambapo kaunti hiyo ni miongoni mwa kaunti 10 zilizo na visa vingi zaidi vya mauaji.

Viwango hivyo vilikadiriwa kwa kuzingatia idadi ya watu wanaoishi katika maeneo ya kaunti, idadi ya vifo vilivyoripotiwa katika ripoti ya takwimu za kitaifa miaka ya 2015 na 2017.

Idadi ya vifo ilizingatiwa katika utafiti huo kwa sababu sio vifo vyote vilivyoripotiwa katika sajili ya kitaifa. Kwa mfano, asilimia 76 ya vifo vyote viliripotiwa na kusajiliwa 2016, idadi ya juu Zaidi nchini. Hata hivyo, idadi ya vifo iliyoripotiwa Mandera na Wajir ilikuwa chini ya asilimia 10.

Kaunti iliyo nambari mbili kwa viwango vya chini vya vifo kati ya watu1,000 ilikuwa Isiolo(6.8) na kufuatwa na Narok(6.9), Kajiado(7.3) na Embu(7.9).
Isiolo ndio kaunti ya pekee ambayo hakuna kisa hata kimoja cha mauaji kiliripotiwa mwaka wa 2016.

Kaunti za Garissa, Mandera na Wajir hazikuzingatiwa katika utafiti huo kwa sababu makadirio ya idadi ya watu 2011 na 2015 yalilandana na hesabu ya watu wote katika uchunguzi wa hesabu ya watu nchini (KNBS) wa 2009.

Hivyo, ni kaunti 44 ambazo zilijumuishwa katika utafiti wa Nation Newsplex.

 

Vifo jijini Nairobi

Ingawa Nairobi ina idadi ndogo zaidi ya vifo nchini, kifo kimoja kati ya 14 mwaka wa 2016 kilitokea jijini, idadi ya juu zaidi.

Hata hivyo, mmoja kati ya watu 10 nchini wanaishi Nairobi, kumaanisha ikilinganishwa na kiwango cha watu cha kitaifa, idadi hiyo ilikuwa ya chini zaidi.

Mwaka wa 2016, jumla ya vifo 189,930 vilisajiliwa, ambavyo vilikuwa takriban asilimia 42 ya vifo vyote mwaka huo ambavyo viliripotiwa bila kusajiliwa(452,214).

Katika miaka sita, Kaunti ya Nyeri iliripoti upungufu mkubwa zaidi wa vifo katika muda wa miaka sita, hadi 2016. Idadi hiyo ilipungua kwa thuluthi moja, hadi tisa, kutoka 14 kwa watu 1,000.

Idadi ya vifo iliongezeka zaidi katika Kaunti ya Elgeyo-Marakwet kutoka 11 hadi 15 kati ya watu 1,000. Kitaifa, idadi ya vifo iliongezeka kwa asilimia 10 hadi 10 kwa watu 1,000 katika kipindi hicho.

Kulingana na Shirika la Afya Ulimwenguni(WHO), uwezekano wa mwanamke Mkenya kuishi hadi miaka 65 ni asilimia 72, kiwango kilichoshuka kwa asilimia 10.

 

Mauaji

Wakati wa kuzingatia kiini cha vifo, Kaunti ya Lamu ilikuwa na idadi ya juu zaidi ya mauaji huku Nakuru na Isiolo zikuwa na viwango vya chini zaidi.

Hii ni kumaanisha kuwa una uwezo mara 58 kufa kutokana na mauaji katika Kaunti ya Lamu ikilinganishwa na Isiolo au Nakuru.

Kulingana na ripoti ya polisi, visa 76 vya mauaji viliripotiwa Lamu, ambapo ni watu 59 kati ya 100,000.

Visa vinane pekee vya mauaji viliripotiwa Nakuru, ambavyo ni chini ya asilimia moja pekee.

Idadi ya mauaji ya kaunti hizo mbili ilikuwa chini zaidi ikilinganishwa na viwango vya kitaifa, cha asilimia sita pekee kwa watu 100,000.

Viwango hivyo kwa kaunti 23 vilikuwa chini ya viwango vya kitaifa vya 6 kati ya watu 100,000.

 

Viini vikuu vya vifo nchini
Pneumonia-vifo 21,295,
Malaria -vifo 16,000
Kansa- vifo 15,762
Ukimwi -vifo 9,471
Ukosefu wa damu mwilini -vifo 8,165

You can share this post!

Uchunguzi waanika uozo unaokumba shule za umma

Kalonzo aandaliwa kuwarithi Uhuru na Raila

adminleo