• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 6:50 PM
Teddy Akumu na timu yake ya Kaizer Chiefs yaduwazwa na wanyonge Nedbank Cup

Teddy Akumu na timu yake ya Kaizer Chiefs yaduwazwa na wanyonge Nedbank Cup

Na GEOFFREY ANENE

Kaizer Chiefs anayochezea Anthony Agay Akumu ilibanduliwa kwenye Kombe la Nedbank baada ya kuduwazwa na Richards Bay 2-1 katika mechi ya raundi ya 32-bora uwanjani FNB, Johannesburg mnamo Jumapili.

Kiungo huyo Mkenya almaarufu kama Teddy Akumu, alikuwa katika kikosi cha kwanza katika mchuano huo ambao Chiefs walijipata bao moja chini dakika ya 29 baada ya Thabani Dube kufuma wavuni kichwa kisafi kutokana na kona.

Beki Siphosakhe Ntiya-Ntiya, ambaye alisababisha kona hiyo akiondosha hatari, alionyeshwa kadi ya njano dakika ya 32 na kuondolewa uwanjani dakika ya 64 alipoongezwa nyingine.

Leonardo Castro, ambaye aliingizwa katika nafasi ya Siphalele Ntshangase mapema katika kipindi cha pili, alisawazisha dakika ya 76. Samir Nurkovic na Dumisami Zuma walishirikiana vyema kabla ya Zuma kuchanjia Castro krosi murwa. Mchezaji wa akiba Siyabonga Vilane alihakikishia Bay tiketi ya raundi ya 16-bora dakika ya 90.

Chiefs inashikilia nafasi ya nane kwenye Ligi Kuu kwa alama 18 kutokana na michuano 15 nayo Bay ni ya pili katika Ligi ya Daraja ya Pili sako kwa bako na viongozi Sekhukhune kwa alama 20 baada ya kusakata michuano 12.

  • Tags

You can share this post!

Ibrahimovic afikisha mabao 500 na kuongoza AC Milan kurejea...

Mama alia kesi yake kuahirishwa