NA PATRICK KILAVUKA
Kocha wa timu ya kikapu ya Umoja Steve Omondi alisema alitumia mbinu ya ulinzi dhabiti na mchezo wa kasi kufunga vikapu hali ambayo ilitumbukiza nyongo matumaini ya wapinzani KU Pirates kwa alama 62-49.
Hii ilikuwa katika Pambano la Ligi ya Kikapu ya Primia (KBF) ambayo iliandaliwa uwanjani UoN, Nairobi, wikendi. Mwanakikapu bora Dolph Benedict wa Umoja alizoa alama 18 ilhali Pirates walivumishwa na Collins Sudi aliyepachika alama 12.
Katika mchuano mwingine wa upande wa akinadada wa Ligi hiyo, KPA iliishinda Eagles Wings 57-26. Madina Akot aliiweka KPA kifua mbele kwa alama 12 ilhali Winnie Wafula aliinua Wings kwa kuzoa pointi 10.
Kocha wa KPA Antony Ojukwu ambaye ameshinda mara 13 akiwa mikobani mwa timu hii, alisema waliweka ulinzi, kutumia nafasi walizopata vyema na kuzoa mpira ambayo wapinzani walizipoteza na kujaza alama.
Naye nahodha KPA Vilima Achieng alikariri kwamba wachezaji wao walicheza kama timu, kutumia uzoefu na kujituma hali ambayo ilizaa matunda zaidi. Na katika Ligi ya Mpira wa Kikapu Daraja ya Pili, NEBULAS ilizoa alama 57 -56 dhid ya NEOSASA.
Mfungaji wa alama nyingi wa NEBULAS alikuwa Clarence Atingo 17 ilhali mchezaji aliyeibuka na alama bora upande wa NEOSASA alikuwa Michael Shimechero alizoa pointi 15.Aidha, mchauno mwingine kati ya MAB walipata ushindi 63-43 mbele ya NEBULAS. Aliyeiweka MAB kifua mbele alikuwa Derrick Owino aliyepachika alama 13 naye Kenneth Salo aliipa matumaini timu ya NEBULAS kwa kuizolea alama 14.