• Nairobi
  • Last Updated May 8th, 2024 8:55 PM
Vihiga Queens inaendeleza rekodi ya kutoshindwa

Vihiga Queens inaendeleza rekodi ya kutoshindwa

Na JOHN KIMWERE

VIHIGA Queens inaendeleza rekodi ya kutoshindwa pia inazidi kukaa kileleni mwa jedwali la Ligi Kuu ya Soka la Wanawake ya Kenya (KWPL) muhula huu.

Vihiga inayosaka kubeba taji hilo kwa mara ya nne ingali kifua mbele baada ya kung’ata Trans Nzoia Falcons kwa mabao 3-0 ugani Kenyatta Stadium, Kitale.  Vihiga ya kocha, Boniface Nyamunyamu ilishusha mchezo safi na kuzoa ushindi kupitia Janet Bundi aliyetikisa wavu mara mbili naye Maureen Ater alitinga bao moja.

”Ninashukuru vipusa wangu kwa ushindi wa alama tatu muhimu hali inayowapa tumaini la kutawazwa mabingwa msimu huu,” kocha wa Vihiga alisema na kuongeza kuwa bado lazima wajitume maana hakuna mteremko.

Nayo Ulinzi Starlets ilidondosha alama mbili ilipotosha bao 1-1 na Wadadia huku Gaspo Women ikiagana sare tasa dhidi mabingwa watetezi, Thika Queens. ”Bora alama moja kuliko kupoteza alama zote lakini ninaamini wachezaji wangu wangejibiidisha wangebeba ushindi baada ya kulemea wapinzani ndani ya vipindi vyote,” kocha wa Gaspo, Domitila Wangui alisema na kuongeza itawabidi wajikaze kwenye mechi zijazo ili kupunguza pengo lililopo kati yao na Vihiga Queens.

Kwenye matokeo mengine, Bunyore Starlets ilitia kapuni alama tatu baada ya kuzoa bao 1-0 dhidi ya Nakuru City Queens nayo Kangemi Starlets ilitoka sare tasa na Kisumu All Starlets.

Katika msimamo wa kipute hicho, Vihiga Queens ingali kifua mbele kwa alama 38, tisa mbele ya Gaspo Women. Ulinzi Starlets inafunga tatu bora kwa alama 27, sawa na Thika Queens tofauti ikiwa idadi ya mabao.

You can share this post!

Mifumo ya teknolojia anayotumia kuendeleza kilimo

Mwaniaji MCA azua ucheshi akidai 2017 alinyimwa fursa...

T L