NA GEOFFREY ANENE
SHULE ya Upili ya Wavulana ya Vihiga ilijiongezea taji la Kombe la Prescott kwenye kabati lake baada ya kupepeta Kisii High 29-8 katika fainali ugani RFUEA mjini Nairobi, Jumapili.
Vihiga, ambayo inafahamika kutoa wanaraga matata Collins Injera, Oscar Ayodi, Edgar Abere, Shaban Ahmed na Collins Shikoli, iliongoza Kisii 7-5 wakati wa mapumziko kabla ya kuzidia wapinzani wao ujanja kabisa katika kipindi cha pili.
Timu hizo zilikuwa zimeshinda makundi yao bila kupoteza.
Kisii walimaliza juu ya Kundi A baada ya kukung’uta Ofafa Jericho 13-12, Maseno 8-6 na Utumishi 6-0.
Waliingia nusu-fainali kutoka kundi hilo pamoja na Ofafa Jericho. Vihiga walitawala Kundi B walipochbanga Jomo Kenyatta 22-7, Mang’u 26-3 na Kangaru 34-0.
Walijikatia tiketi ya nusu-fainali pamoja na Jomo Kenyatta. Kisii ilitinga fainali baada ya kulipua Jomo Kenyatta 18-0 nao Vihiga, ambao Agosti walinyakua taji la raga ya wachezaji saba kila upande ya shule za upili, walizima Ofafa 24-5.
Mabingwa wa makala yaliyopita Upper Hill hawakushiriki mwaka huu. Mashindano hayo yalifanyika majuma machache baada ya wasichana ambayo St Mary’s Mabera kutoka Migori ilinyamazisha Eregi kutoka Kakamega 14-10 katika fainali mjini Nakuru.