• Nairobi
  • Last Updated March 29th, 2024 4:10 PM
Wamaasai wanavyovumisha utalii kupitia sherehe za Moran

Wamaasai wanavyovumisha utalii kupitia sherehe za Moran

Na GEORGE SAYAGIE

KAUNTI ya Narok inatarajiwa kuwa kivutio kikubwa cha utamaduni kwa miezi mitatu hadi minne ijayo, ukoo wa Purko miongoni mwa jamii ya Wamaasai unapojitayarisha kwa hafla ya kuwaingiza vijana wa Moran kwenye utu uzima.

Hafla hiyo huwa inafanyika mara moja kila baada ya miaka kumi, na huwa hatua muhimu kwa vijana hao.Kabla vijana kuvuka rika, huwa kuna shughuli kadhaa ambazo hufanywa kama njia ya kuwatayarisha.

Baadhi yazo ni kuwanyoa nywele, wavulana kufunzwa masuala na mienendo ya utu uzima na hafla nyingine, ambapo huwa wanakula nyama pamoja.

Ulaji nyama pamoja miongoni mwao huashiria mwisho wao kuwa wavulana na mwanzo wa maisha mapya kama watu wazima.Kufikia sasa, tarehe ambapo hafla yenyewe itafanyika bado haijatangazwa.Hafla hiyo huwavutia maelfu ya watalii kutoka humu nchini na nchi za nje kutokana na upekee wake wa kitamaduni.

Mnamo Jumapili jioni, mamia ya Wamorani kutoka vijiji vya Melili katika maeneo ya Narok Kusini na Kaskazini waliingia mjini Narok kwa kishindo.

Wamorani hao walikuwa wamebebwa kwa pikipiki na magari, huku wakipiga vuvuzela.Waliigeuza taswira ya mji huo kuwa nyekundu kutokana na rangi ambazo huwa wamepaka nywele zao.

Msafara huo ni sehemu ya misafara kadhaa kama hiyo ambayo imeshuhudiwa mjini humo kwa muda wa majuma mawili yaliyopita.Wamorani hao wamekuwa wakielekea katika eneo maalum katika kijiji cha Rotian, Narok Kaskazini, ambako shughuli maalum ya kuwanyoa nywele itafanyika katika muda wa miezi mitatu ijayo.

Hafla hiyo huitwa Eunoto kwa lugha ya Kimaasai.Wamorani wote watanyolewa baada ya nywele zao kumwagiliwa maziwa, wakiwa wamekalia kiti chenye miguu mitatu.

Baada ya hatua hiyo, watashirikishwa kwa hafla ya kuwatawaza kama watu wazima.Kiongozi wa Wamorani hao, Bw Amos Ole Tikani alisema bado wanatarajia kuwapokea wengine wengi zaidi.

“Kufikia sasa, tumepokea Wamorani kutoka makundi tisa ambako ukoo huo huwa unaishi. Wanatoka katika maeneo kama Nkaretta, eneo la Mau katika Narok Kaskazini, Naroosura katika Narok Kusini na Mosiro katika Narok Mashariki. Watakuwa miongoni mwa Wamorani 6,000 wanaojitayarisha kwa hafla hiyo. Wanatarajiwa kula mafahali 3,000 na mbuzi na kondoo 30,000,” akasema.

Bw Joseph Ole Yenko, ambaye ni chifu wa kitamaduni wa jamii hiyo na anayewaongoza Wamorani kutoka eneo la Melili, alisema hafla hiyo inachukuliwa kwa uzito sana na jamii ya Wamaasai. Aliitaja kuwa “nguzo kuu” kwa maisha ya kila mtu kutoka jamii hiyo.

“Hafla inajumuisha ujenzi wa Manyatta, uteuzi wa viongozi, uchezaji densi, unyoaji nywele, ulaji nyama na utoaji baraka kwa washiriki wote,” akasema Bw Yenko.Hafla hiyo huhusisha vijana kutoka jamii hiyo walio kati ya umri wa miaka 15 na 30.

You can share this post!

Taabani kwa kutisha kumuua Rais Kenyatta

TAHARIRI: Mswada wa Duale usipingwe ovyo