• Nairobi
  • Last Updated April 20th, 2024 7:55 AM
Wamalwa aapa kubeba Homeboyz Prinsloo 7s

Wamalwa aapa kubeba Homeboyz Prinsloo 7s

Na GEOFFREY ANENE

CHIPUKIZI Amon Wamalwa ameapa kuendelea kuongoza Homeboyz kutesa kwenye raga za kitaifa za wachezaji saba kila upande zitakazoingia duru ya tano wakati wa Prinsloo Sevens mnamo Julai 9-10 mjini Nakuru.

Wamalwa alichangia pakubwa katika ushindi wa Homeboyz wa duru ya nne Dala Sevens mjini Kisumu wikendi iliyopita. Aliibuka mfungaji bora wa miguso (tisa) na pointi (60) pamoja na kunyakua tuzo ya mchezaji bora.

Kwenye droo ya Prinsloo iliyofanywa Jumatano, Homeboyz itakabana koo na Catholic Monks, Kabras Sugar na Western Bulls katika Kundi A.

Menengai Oilers, Chuo Kikuu cha Masinde Muliro, Nakuru na Kisumu ziko Kundi B, viongozi wa ligi hii KCB pamoja na Nondescripts, Impala na Kenya Harlequin wako Kundi C nao Mwamba, Strathmore Leos, Blak Blad na Vihiga Granites walitiwa Kundi D.

“Tumekutana na wapinzani wote ambao tumekutanishwa nao Prinsloo kwa hivyo vitakuwa vita vya ubabe. Hata hivyo, tutachukulia kila mechi kwa uzito,” alisema.

Wamalwa aliongeza, “Malengo yangu ya Prinsloo ni kusaidia timu yangu kuhifadhi taji. Pia, nataka nifagie tuzo nilizoshinda Dala Sevens. Tuko tayari kunguruma tena.”

Duru nne za kwanza zimeshuhudia washindi wanne tofauti ambao ni KCB (Kabeberi Sevens), Strathmore Leos (Christie Sevens), Mwamba (Driftwood Sevens) na Homeboyz (Dala Sevens).

  • Tags

You can share this post!

Korti yakataa kumzuia Samboja kutetea kiti chake

Askofu awaita walevi kanisani wapate mafundisho ya kidini

T L