• Nairobi
  • Last Updated March 29th, 2024 6:50 AM
Wanahabari 250 wamo jela kote duniani – Ripoti

Wanahabari 250 wamo jela kote duniani – Ripoti

Na MASHIRIKA

MATAIFA ya Misri, Eritrea na Cameroon yanaongoza kwa kudhulumu wanahabari barani Afrika.

Kulingana na ripoti ya Kamati ya Kimataifa ya Kulinda Wanahabari (CPJ) ya mwaka huu, idadi kubwa ya wanahabari wamefungwa gerezani katika mataifa hayo matatu.

Wanahabari 26 walifungwa gerezani mwaka huu nchini Misri kwa madai ya kueneza habari za uongo na kuchochea ugaidi.

Wengi wa wanahabari nchini Misri walikamatwa kufuatia maandamano makubwa yaliyofanyika Septemba 19 ambapo raia wa nchi walilalamikia ongezeko la ufisadi jeshini na kumtaka Rais Abdul Fattah al-Sisi kujiuzulu.

Wanahabari 16 walisukumwa gerezani nchini Eritrea, Cameroon (7), Burundi (4), Rwanda (4), Nigeria (1), Chad (1), Comoros (1), DR Congo (1), Sudan Kusini (1), Ethiopia (1), Tanzania (1) na Somalia (1).

Kulingana na ripoti ya CPJ, China na Uturuki zinaongoza kwa kutatiza uhuru wa wanahabari kote ulimwenguni.

Katika ukanda wa Mashariki ya Kati, Saudi Arabia inaongoza kwa kuwafunga wanahabari bila hatia.

Ripoti ya CPJ inaonyesha kuwa wanahabari 250 wamefungwa kote duniani. Ripoti ya 2018 ilionyesha kuwa wanahabari walikuwa gerezani kote ulimwenguni. Mwaka wa 2016 ulivunja rekodi kwa kuwa na jumla ya wanahabari 273 waliokuwa wanatumikia vifungo vya jela.

Kimataifa, China inaongoza kwa kuwa na idadi kubwa ya wanahabari wanaotumikia vifungo magerezani ikifuatiwa na Uturuki, Saudi Arabia, Misri, Eritrea, Vietnam na Iran.

Wengi wa wanahabari hao waliofungwa wanakabiliwa na makosa ya kueneza habari za ‘uongo’ dhidi ya serikali.

Kulingana na ripoti, idadi ya wanahabari ambao wamefungwa kwa ‘kueneza habari za kupotosha’ imeongezeka hadi 30 mwaka huu ikilinganishwa na 28 mwaka jana.

Mwaka jana, mataifa ya Urusi na Singapore yalipitisha sheria ya kupiga marufuku uchapishaji wa habari za kupotosha.

Wanahabari 47 wamefungwa gerezani nchini Uturuki mwaka huu ikilinganishwa na 68 mwaka jana.

Rais Recep Tayyip Erdo?an mwaka jana alifunga vituo 100 vya habari na kufikisha mahakamani wafanyakazi wake kwa madai ya kuendeleza ugaidi.

Serikali ya Uturuki mnamo Oktoba ilipitisha sheria iliyoruhusu wafungwa waliopatikana na hatia ya kueneza habari za kupotosha na propaganda kukata rufani..

Wengi wa wanahabari wanaozuiliwa nchini humo wamekata rufani na kesi zao zinaendelea kusikizwa wakiwa kizuizini.

Ripoti ya CPJ ya 2019, imebaini kuwa wanahabari 48 wamezuiliwa gerezani nchini China.

You can share this post!

JAMHURI DEI: Wakenya nchini Canada kujumuika kuadhimisha...

Vipusa wahamia kwa polo mkora

adminleo