Na MASHIRIKA
MFUMAJI Wilfried Zaha alifunga mabao mawili na kusaidia waajiri wake Crystal Palace kupepeta Aston Villa 3-1 katika Ligi Kuu ya Uingereza (EPL) mnamo Jumamosi ugani Selhurst Park.
Villa walijiweka uongozini katika dakika ya tano kupitia bao la Ollie Watkins aliyemwacha hoi kipa Vicente Guaita. Hata hivyo, Palace walisawazisha mambo chini ya dakika tatu kupitia kwa Zaha aliyemzidi ujanja beki Ezri Konsa na kipa Emiliano Martinez.
Bao ambalo Jeffrey Schlupp alifungia Palace katika dakika ya 26 halikuhesabiwa baada ya teknolojia ya VAR kubaini kuwa Odsonne Edouard alikuwa ameotea kabla ya Schlupp kucheka na nyavu za wageni wao.
Palace walifungiwa penalti na Zaha baada ya Lucas Digne kunawa mpira uliopigwa na Marc Guehi Kum. Ushirikiano mkubwa kati ya Zaha na
Eberechi Eze ulichangia bao la tatu la Palace ambalo lilijazwa kimiani na Jean-Philippe Mateta.
Zaha, 29, sasa anajivunia jumla ya mabao 12 katika EPL tangu mwaka wa 2022 na amefikia rekodi ya Luka Milivojevic ambaye amewahi kupachika wavuni idadi kubwa zaidi ya magoli katika mwaka mmoja kambini mwa Palace.
TAFSIRI NA: CHRIS ADUNGO