• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 1:29 PM
KIPAJI: Aanzisha shule ya kutoa mafunzo ya usanii

KIPAJI: Aanzisha shule ya kutoa mafunzo ya usanii

Na MAGDALENE WANJA

KWA vijana wengi, kozi katika somo la kibiashara la uagizaji bidhaa na huduma – procurement – ni mojawapo ya njia za kuwa na uhakika wa kupata kazi nzuri, hasa nchini Kenya.

Hata hivyo, kwa Cane Mjomba ambaye ni DJ mjini Nakuru alifanya kozi hiyo ya kibiashara kuwafurahisha tu wazazi wake.

“Baada ya kujisajili kufanya kozi ya diploma katika somo la kibiashara katika Kenya Institute of Management (KIM), nilijua kuwa baada ya kufuzu nitapata kazi nzuri,” anasema Mjomba.

Akiwa chuoni, alianza kupata hamu ya ujuzi na kufanya kazi kama DJ, jambo lililomfanya kuanza mazoezi katika taaluma hiyo.

Alijifunza kwa kutumia vifaa alivyokodi kutoka kwa marafiki zake na wakati mwingine alitumia kompyuta yake kujifunza kwa kutumia programu ya VirtualDJ.

Cane Mjomba (kushoto) ni DJ mjini Nakuru. Hapa anamwelekeza mmoja wa wanafunzi wake. Picha/ Magdalene Wanja

“Nilikuwa na hamu sana ya kujifunza kwani nilianza kuazima vifaa hivyo kwa Sh400 kwa siku ili kujipa muda zaidi wa kujifunza,” akasema Mjomba wakati wa mahojiano.

Baada ya kukamilisha masomo yake mnamo mwaka 2015, alipata kazi katika idara ya Posta ambayo ilikuwa fahari kwake na kwa wazazi wake.

Kulingana na Mjomba, kazi hiyo ilimsaidia kuishi maisha mazuri ila haikumpa raha.

Alianza kuifanya kazi ya DJ mnamo wikendi. Ni kazi ambayo ilimpa hela zaidi.

“Nilifanya kazi katika Posta kwa muda wa miezi sita na baada ya hapo nikaiacha kwani nilitaka kuwa DJ,” akasema Mjomba.

Cane Mjomba ni DJ mjini Nakuru. Picha/ Magdalene Wanja

Alipata kazi katika maeneo ya burudani, sherehe kama vile harusi na mikutano ya aina mbalimbali.

Mnamo mwaka 2018, alianzisha shule ya kutoa mafunzo ya usanii ya kuwapa nafasi vijana kujifunza taaluma hiyo.

“Nilianzisha chuo cha mafunzo ili kuziba pengo kubwa lililokuwa kwani vijana wengi walisema kuwa hawakupata nafasi ya kujipatia ujuzi huo,” akasema Mjomba.

Chuo chatoa mafunzo

Chuo hicho hicho kinachojulikana kama Blueray DJ Academy kinatoa mafunzo kwa vijana na wazee wachache ambao wana hamu ya ujuzi huo.

Kozi nzima katika chuo hicho inachukua muda wa miezi miwili katika vitengo kama vile scratching, music blending, beat-matching na masomo ya darasani.

Karo ya kozi nzima ni Sh25,000 ila kuna baadhi ya wanafunzi ambao hulipia kozi zao kwa mpango wa malipo kila siku.

“Kuna kitengo cha watu ambao wana ujuzi ila wangetaka ujuzi zaidi, hao hulipa karo ya Sh15,000,” akasema Bw Mjomba.

Kila mwezi, Mjomba anaweza kupata faida ya kati ya Sh100,000 na Sh150,000 ambazo ni mara tatu ya mshahara aliopata katika kazi yake ya hapo awali.

Anasema kuwa japokuwa wazazi wake walipinga sana hatua yake ya kuacha kazi, baadaye walimuunga mkono baada yake kuwaelezea nia yake.

“Kwa muda wa miaka mitano ya usoni, nina ndoto ya kuanzisha shule za mafunzo ya usanii katika miji mingine nchini,” akasema Mjomba.

You can share this post!

Ghana yazimia Kenya ndoto ya kufuzu magongo Olimpiki

SHINA LA UHAI: Changamoto ya majitaka katika miji yetu

adminleo