Habari

Serikali yapiga marufuku maudhui ya kisiasa katika tamasha za shule

Na ELVIS ONDIEKI April 7th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

SHERIA zinazoongoza Tamasha za Kitaifa za shule zimebadilishwa ambapo sasa ni marufuku kuwa na mawasilisho yenye mada za kisiasa.

Imebainika sheria hiyo iliwekwa kuelekea Tamasha za Kitaifa za Muziki na Filamu zinazoanza leo katika Chuo cha Mafunzo cha Walimu cha Kagumo, Kaunti ya Nyeri.

Wanafunzi watawasilisha mushairi, densi na sanaa nyingine wakati wa tamasha hizo zinazotarajiwa kusisimua mno.

Sheria mpya inaonya dhidi ya kuwa na wasilisho ambalo linazungumzia siasa, ajenda ya kisiasa, kampeni au kuwa na mada inayowakejeli watumishi wa umma.

Huenda sheria hiyo imeanzishwa kutokana na kisa cha mwaka jana ambapo Wasilisho la Echoes of War la Butere Girls lilizua utata kati ya serikali na usimamizi wa shule hiyo.

Mchezo huo wa kuigiza ulikuwa umeandikwa na Seneta wa zamani wa Kakamega Cleophas Malala ambaye ni naibu kiongozi wa DCP, hasimu mkubwa wa Rais Ruto.

Wakati huo Rais William Ruto aliashiria kuwa kamba itakazwa zaidi kuhusiana na mawasilisho katika tamasha za muziki.

“Kuna mengi ya kujivunia kama taifa kuliko kuwa na mtazamo hasi kuhusu kila kitu. Kama Rais, sitakubali taifa litumbukizwe kwenye chuki na ghasia kutosholeza ajenda ya viongozi wenye ajenda yao,” akasema Rais Ruto.

“Nawaomba wanasiasa wetu waachane na watoto wetu na wapeleke siasa zao kwingine. Tuko tayari kupambana nao katika mawanda ya kisiasa,” akaongeza.

Hata hivyo, wakati huo hakutaja shule au mwanasiasa yeyote.

Sheria hiyo mpya tayari imewaondoa washindi wa kitengo cha uigizaji mwaka jana Moi High School Mbiruri kutoka Kaunti ya Embu.

Duru ziliarifu Taifa Leo kuwa mchezo wao ulionekana kuenda kinyume cha sheria hiyo baada ya kuzungumzia Singapore.

“Mchezo huo haukuruhusiwa kwa sababu ulijikita katika suala zima la Kenya kuchukua mkondo ambao utaiwezesha kufikia hadhi ya mataifa kama Singapore,” duru hizo zikaarifu.