• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 7:00 PM
Madiwani waliokataliwa na wapigakura kuchunguzwa na EACC

Madiwani waliokataliwa na wapigakura kuchunguzwa na EACC

Na PETER MBURU

TUME ya Maadili na Kupambana na Ufisadi (EACC) Jumatatu imeandikia wawakilishi wadi wanane wa Kaunti ya Busia wa zamani kufika mbele yake kuhusiana na sakata ya ufisadi kwenye bajeti ya ziada kaunti hiyo.

EACC iliwaandikia madiwani hao Jumatatu asubuhi ikiwataka kufika mbele yake Septemba 12 ili wahojiwe kuhusiana na sakata hiyo, kwa barua zilizoelekezwa kwa karani wa bunge na katibu wa kaunti.

“Tunachunguza madai ya ufisadi na kughushi kuhusiana na bajeti ya ziada ya kaunti,” ikaandika tume hiyo.

Madiwani wanaotarajiwa kupigwa msasa na tume hiyo sasa ni  Philip  Emaset, Tony Opondo, Josephat Wandera, Stephen Ajakait, Godfrey Odongo, Gabriel Okello, Kenneth Ichasi na Margaret Chale.

Hii ni miezi mitatu baada ya gavana wa kaunti hiyo Sospeter Ojaamong pamoja na maafisa wengine wa kaunti kushtakiwa kwa kupotea kwa Sh8milioni mnamo Juni.

Gavana Ojaamong pamoja na waliokuwa mawaziri Bernard Yaite, Allan Ekweny, na Samuel Ombui aliyekuwa wa fedha walikamatwa na kushtakiwa Juni ambapo walikana makosa ya kushirikiana kutekeleza makosa ya kiuchumi, matumizi mabaya ya afisi na kufanya mradi ambao haukuwa umepangwa kwenye bajeti.

Aidha, takriban mwezi uliopita, aliyekuwa gavana wa Nyandarua Daniel Waithaka Mwangi pamoja na afisa mwingine mkuu wa kaunti walishtakiwa kwa sakata za kupotea kwa pesa za umma walipokuwa ofisini.

You can share this post!

Senegal vs Madagascar: Shabiki afariki kabla ya mechi

AFCON: Kundi F la Kenya sasa li wazi

adminleo