• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 5:22 PM
Raila na Ruto wateka mageuzi ya Katiba

Raila na Ruto wateka mageuzi ya Katiba

Na BENSON MATHEKA

WITO wa kura ya maamuzi ili kufanyia Katiba marekebisho, umegeuka safu mpya ya vita vya ubabe kati ya Naibu Rais William Ruto na kiongozi wa chama cha ODM Raila Odinga. Hii inaibua maswali kuhusu iwapo mabadiliko yanayokusudiwa yanalenga kufaidi mwananchi wa kawaida ama wanasiasa.

Viongozi hao wawili wameonekana kuteka mjadala kuhusu marekebisho hayo, na kufanya suala hilo kuchukua mkondo wa siasa za mgawanyiko zinazolenga hasa uchaguzi mkuu wa 2022.

Imeibuka kuwa Bw Ruto na Bw Odinga wanachukua fursa hii kujipigia debe kwa kutaka wananchi wawaone kama wanaowajali kwa kusukuma wapunguziwe mzigo wa maisha unaotokana na mahitaji ya Katiba ya sasa, ambayo imebuni nyadhifa nyingi za uongozi zenye gharama kubwa.

Wakiandamana na wandani wao, Bw Odinga na Bw Ruto wamekuwa wakizunguka nchini wakitoa misimamo tofauti kuhusu kura hiyo, kila mmoja akivutia kwake.

Ingawa Bw Odinga amekuwa akidai kwamba mabadiliko ya Katiba ni miongoni mwa masuala aliyokubaliana na Rais Kenyatta, Bw Ruto amekuwa akidai kwamba kiongozi huyo wa ODM analenga kutumia kura ya maamuzi kubuni nyadhifa mpya serikalini.

Awali, Bw Ruto alikuwa amepinga kufanyika kwa kura hiyo lakini juzi alishangaza wengi alipobadilisha msimamo na kuunga mkono.

Kufikia sasa, wanasiasa hao wawili na wandani wao wamegawanyika kuhusu masuala yanayofaa kushirikishwa kwenye kura ya maamuzi ili kupigiwa kura.

Kambi ya Bw Ruto inasisitiza kuwa kuna viongozi wanaotaka kura hiyo iwe ya kubuni nyadhifa mpya ili kufaidi wanasiasa wachache katika kile wanachodai ni kuhusisha Wakenya wote serikalini.

Akiongea akiwa Meru siku moja baada ya kukubali kura ya maamuzi, Bw Ruto alisema atakubali kura ya maamuzi inayolenga kupunguzia raia mzigo wa kupanda kwa gharama ya maisha.

“Ikiwa wale wanafikiri watatumia kura ya maamuzi kubuni nyadhifa mpya tunawaambia wasahau,” Bw Ruto alisema.

Bw Odinga naye amekuwa akipendekeza mfumo wa ugatuzi unaohusisha viwango vitatu kwa kubuni maeneo 16 badala ya kaunti 47 zilizopo kwa wakati huu.

Pendekezo hili tayari limepingwa na wengi wakidai mfumo wa ugatuzi wa sasa umefaidi Wakenya mashinani na haufai kubadilishwa.

Wandani wa Bw Odinga wamekuwa wakipendekeza mfumo wa serikali ya bunge ambao utakuwa na waziri mkuu na manaibu wake wawili.

Ingawa walikaribisha hatua ya Bw Ruto ya kukubali kura hiyo, wanasiasa wanaomuunga Bw Odinga wanasema Naibu Rais hafai kutoa masharti kuhusu yanayopaswa kushirikishwa na pia wanasisitiza kukubali kwake kuna unafiki ndani yake.

Malumbano ya viongozi hao na wandani wao yanaonyesha kuwa wanasiasa wanalenga kutimiza malengo yao ya kibinafsi.

Kwa upande mwingine wananchi wameonekana kutazama tu huku mashirika ya kijamii na kitaaluma yakikaa kimya.

Ni Baraza la Kitaifa la Makanisa (NCCK) ambalo limejitokeza wazi kujadili suala hili. Baraza hili linaunga pendekezo la kubuniwa kwa wadhifa wa waziri mkuu lakini linaunga kupunguzwa kwa viti vya uwakilishi. Kulingana na katibu mkuu wa NCCK Canon Peter Karanja, idadi ya mawaziri pia inafaa kupunguzwa.

Lakini muungano wa mashirika ya kijamii (CSRG) unaonya kuwa pendekezo la kupunguza idadi ya wawakilishi halifai kulenga wanawake na vijana katika juhudi za kupunguza gharama ya maisha katika serikali kuu na serikali za kaunti.

Mshirikishi wa shirika hilo Suba Churchil anasema kwamba madai kwamba wawakilishi wa wanawake wanaongeza gharama ya serikali hayana msingi.

Kulingana na Bw Churchil, Seneti haifai kufutiliwa mbali kama baadhi ya watu wanavyopendekeza.

You can share this post!

VASCO DA GAMA: Kitega uchumi cha Malindi kilicho hatarini...

Obado Mkenya wa kwanza kushtakiwa kwa mauaji ya mtoto...

adminleo