• Nairobi
  • Last Updated March 29th, 2024 5:46 PM
Wabunge kuamua tarehe mpya ya uchaguzi

Wabunge kuamua tarehe mpya ya uchaguzi

Na DAVID MWERE

WABUNGE Jumatano wataupigia kura mswada unaopendekeza tarehe ya uchaguzi mkuu ujao ibadilishwe kutoka Jumanne ya pili ya mwezi Agosti hadi Jumatatu ya kwanza ya mwezi Disemba, hali itakayoongeza muda wao ofisini kwa miezi minne.

Mswada huo wa Marekebisho ya Katiba 2017 unadhaminiwa na Mbunge wa Kimilili, Dkt Chris Wamalwa na itahitaji theluthi mbili ya wabunge kuupitisha, hii ikiwa ni wabunge 233 kulingana na katiba.

Kwa mujibu wa mbunge huyo wa chama cha Ford Kenya, mswada wake unaugwa mkono na idadi kubwa ya wabunge wenzake.

Anasema kwamba karibu wabunge 250 wamemhakikishia kuwa wataupitisha wakati wa kuupigia kura saa nane mchana.

“Sina shaka kwamba mswada huu utapitishwa kwa sababu ninaungwaji mkono wa wenzangu wengi,” akasema Dkt Wamalwa.

Alisisitiza kwamba tarehe ya uchaguzi lazima iheshimu tamaduni na mienendo zilizizokuwepo kabla ya kurasmishwa kwa katiba mpya.

Iwapo utapitishwa, mswada huo pia unatarajiwa kuathiri uchaguzi wa maseneta, wawakilishi wadi, magavana na urais ambao pia watasalia mamlakani kwa miezi minne zaidi.

Sababu nyingine anayoitaja Dkt Wamalwa ya kutaka mabadiliko hayo yatekelezwe ni mitihani na kitaifa ya KCPE na KCPE inayoandaliwa mwezi Oktoba na Novemba, akisema kura za mwezi Agosti huathiri masomo ya watahiniwa haswa kukiandaliwa uchaguzi wa marudio jinsi ilivyokuwa mwaka jana.

Hata hivyo, kikwazo kikuu ni hitaji la sheria kwamba mabadiliko hayo yatakumbatiwa tu kupitia kuandaliwa kwa kura ya maamuzi kwa kuwa kubadilishwa kwa tarehe ya kura pia husogesha muda wa kuhudumu kwa rais.

Kikwazo kingine ni gharama ya kura ya maoni inayokadiriwa kuwa Sh12 bilioni kulingana na Tume ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC), ambayo kwa sasa haiwezi kuwajibika kikamilifu baada ya makamishina wanne kujiuzulu mwaka jana na bado nafasi zao hazijajazwa.

Mswada kama huo ulikataliwa mwaka wa 2014 ulipowasilishwa na aliyekuwa Mbunge wa Ugenya, Bw David Ochieng.

You can share this post!

Obado Mkenya wa kwanza kushtakiwa kwa mauaji ya mtoto...

TAHARIRI: Wadau washirikiane kufanikisha mitihani

adminleo